Monday, July 16, 2012

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI YA UPINZANI MHE MCHUNGAJI ISRAEL YOHANA NATSE (MB) WIZARA YA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2012/2013


1.     Utangulizi
Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kusimama hapa mbele ya Bunge hili, kuwasilisha   maoni na mapendekezo ya Kambi ya Upinzani kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka 2012/2013 kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Bunge, kanuni ya 99(7).

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa shukrani za kipekee kwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Mhe. Freeman Aikael Mbowe (Mb) kwa imani yake kubwa kwangu na kuniteua kuwa Waziri Kivuli wa Wizara hii. Nami natoa ahadi kwake kuwa nitajitahidi  kwa kadri ya uwezo wangu na kwa jinsi Mwenyezi Mungu atakavyonijalia, natumaini kwa uwezo wake nitatimiza matarajio yake kwangu.
Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa naomba kutoa shukrani zangu za dhati kwa Dr.Willbrod Peter Slaa-Katibu Mkuu wa CHADEMA, mbunge wa miaka 15 wa Jimbo la Karatu, kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuiongoza CHADEMA na kutupa miongozo ya namna ya kuwa wabunge mahiri, sambamba na kuwa mawaziri vivuli hasa.
Mheshimiwa Spika, napenda kuishukuru familia yangu kwa imani na uvumilivu waliouonesha wakati wote ambao ninakuwa mbali nao nikiwa  katika shughuli za ujenzi wa Taifa. Maombi yenu ni muhimu.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sijatenda haki kwa wananchi wa Jimbo la Karatu kama sitawashukuru kwa imani kubwa waliyo nayo kwangu na kwa chama changu cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), nami nawaahidi kuwa nitaitunza na kuiheshimu imani yao kwangu, kuendelea kushirikiana nao kuleta maendeleo katika Jimbo na Wilaya yetu na mwisho kukifanya CHADEMA kuwa chama kiongozi kwa wilaya na kwa nchi nzima katika uchaguzi wa mwaka 2015. Asanteni Sana.
Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza wananchi wa vijiji vya Kiburumo, Kongwa na Nyarutanga waliofanya uchaguzi wao jana na kauli moja kupitia sanduku la kura wameipatia CHADEMA ushindi mkubwa wa kuongoza Serikali katika vijiji hivyo, chini ya Mwenyekiti Juma Hamza-Kiburumo, Juma Iddi Kibali- Kongwa na Changanya Midenge-Nyarutanga. Hizo ni mvua za vuli masika inakuja. Tunasema hivi (The sun never set in CHADEMA) CHADEMA hakuna kulala mpaka kieleweke.

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini kwa umuhimu mkubwa nawashukuru waheshimiwa wabunge wote wa Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na Kamati nzima ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa ushauri na ushirikiano mkubwa walionipatia katika utendaji wangu kazi ndani na nje ya Bunge. Asanteni sana!


2.     Umuhimu wa Ulinzi na Usalama katika Nchi Yetu
Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kwamba nchi inapokuwa salama ndipo watu wake huweza kuishi kwa amani na utulivu. Amani na utulivu vinapotawala katika nchi, watu wake huwa na uhuru wa kufanya shughuli mbalimbali kwa ajili ya kujipatia mahitaji yao ya kila siku na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa nchi yao.
Mheshimiwa Spika, Tanzania imekuwa ikisifika duniani kwa kudumisha amani hadi kuitwa “Kisiwa cha Amani”. Mwezi Agost 2000, Rais Mstaafu wa Marekani Bill Clinton aliuita Mji wa Arusha kuwa ni “Geneva of Afrika” kutokana na mji huo kuwa ni kitovu cha usuluhishi na upatanishi wa migogoro ya kimataifa. Hii ni sifa kubwa kwa Tanzania kwa kuaminiwa na mataifa mengine kuwa ni “Mlinzi wa Amani”.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inataka Serikali ielewe kwamba amani haipatikani kwa kutokuwa na vita katika nchi tu, ila amani huongezeka kama wananchi wanapata mahitaji yao ya msingi ambayo huwafanya waishi maisha ya staha. Amani huendelea kuimarika na kukomaa iwapo nchi itakuwa inatawaliwa kwa misingi ya haki, sheria na usawa katika mgawanyo wa rasilimali za nchi kwa faida ya wananchi wake wote.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inatambua na inaheshimu vyombo vya Ulinzi na Usalama katika kulinda na kudumisha amani ya nchi yetu. Kambi inatambua vilevile kuwa ni kazi ngumu zaidi  kuwalinda watu wasio na amani mioyoni mwao kutokana na kukosa haki zao za msingi. Hivyo ni dhahiri kuwa amani ya kweli ya nchi yetu itakuwepo na itaendelea kuwepo endapo Serikali iliyopo madarakani na Serikali itakayokuwa madarakani itatafuta kwanza amani ya nafsi za watu kwa kuwatimizia mahitaji yao ndipo kazi ya ulinzi wa amani katika nchi itakuwa rahisi.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaamini kabisa kuwa Jeshi ni chombo huru ambacho hakitakiwi kuwa na itikadi ya chama chochote cha siasa au kuwa na mlengo wowote wa imani ya kidini. Lakini kwa masikitiko makubwa ni kwamba sasa hivi wanasiasa wameanza kuingilia mchakato mzima wa uajiri wa wanaojiunga na jeshi hilo. Hili limekuwa linaharibu sifa kubwa ya jeshi letu, jambo linaloweza kugawa jeshi kwa misingi ya uchama. Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kuachia Jeshi lenyewe mchakato mzima wa uajiri kwa kulingana na matakwa ya jeshi lenyewe kuliko shinikizo la wanasiasa kuingiza watoto wao, jamaa zao na watoto wa rafiki zao.
3.0 Mapitio ya Utekelezaji wa Bajeti 2011/2012
Mheshimiwa Spika, kwa ujumla fedha iliyoidhinishwa kwa Wizara hii ilitolewa kwa kiwango cha kuridhisha isipokuwa fedha ya maendeleo ilikuwa ni asilimia 40% tu ya fedha iliyoidhinishwa na bunge. Hii haileti taswira nzuri, kwani maendeleo katika wizara hii yako chini ya wastani.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Kamati ya Bunge ya tarehe 7 Juni, 2012 ni kwamba fungu 57 Ulinzi lilipokea shilingi bilioni 129. Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 30 ni fedha maalum (ring fenced) kwa ajili ya kununua meli za kivita, ambao mchakato wake umeanza na unatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2012. Kambi ya Upinzani tunaitaka serikali ihakikishe kuwa ahadi hii inatimia kwa maslahi ya ulinzi wa taifa letu.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Ulinzi kwa kamati ya bunge changamoto inayoathiri bajeti ya Wizara ya Ulinzi ni kuchelewa kutolewa kwa fedha kutoka hazina kwa wakati, jambo ambalo limesababisha kushindwa kutekeleza baadhi ya majukumu yake kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, tuapenda kusisitiza kwamba Serikali iepuke urasimu kwa mambo yanayohusu ulinzi na usalama wa nchi yetu. Kama bajeti imepitishwa na bunge, jambo la kufanya ni kutoa fedha hizo kwa wakati ili kutekeleza majukumu yaliyopangwa.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa zilizopo gharama za kuondoa matrekta bandarini kwa mwaka 2011/2012 zilitumika jumla ya shilingi 4,048,325,331. Hakika fedha hizi ni nyingi sana kwa kazi ya kuondoa tu matrekta bandarini.
Kambi ya Upinzani, inataka kupata majibu ni Matrekta mangapi yaliondolewa na gharama ya kuondoa trekta moja ilikuwa kiasi gani? Na gharama hizo zilikuwa ni kwa ajili ya shughuli gani haswa?
4.0            Vyombo vya Ulinzi na Usalama na Wajibu wake kwa Wananchi
Mheshimiwa Spika, madhumuni ya vyombo vya ulinzi na usalama ni kuwalinda raia wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ila kinyume na dhamira hiyo, uzoefu hapa kwetu Tanzania inaonekana kama vile vyombo hivi ni kwa ajili ya kuilinda Serikali. Ni kweli kwamba vyombo hivi vina jukumu pia la kuilinda Serikali, lakini kuna baadhi ya matukio ambayo inaonekana dhahiri vyombo hivi vikiacha jukumu la kuwalinda raia na badala yake kuwapiga na kuwanyanyasa raia.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa  taarifa  ya “Tanzania Land Alliance” (TALA) ya tarehe 30 Machi 2012 inasemekana kwamba  mnamo tarehe 17 Machi, 2012 askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) waliwaua kwa kuwapiga risasi watu watano na kuwajeruhi wengine watatu katika eneo la  Maguba, Kitongoji cha Lupemenda, Kijiji cha Kiwale, Kata ya  Igawa, Tarafa ya Malinyi wilayani Ulanga.
Mheshimiwa Spika, katika tukio hili watu waliopoteza maisha ni Sanyiwa Ndahya (28), Lutala Ndahya (45), Kulwa Luhende (48), Ng’erebende Nchambi Lukuresha (26) na Kashinje Msheshiwa (35).
 Waliojeruhiwa ni Zina Msheshiwa (29), Msheshiwa Ndahya (53), Khama Chisongelile Tiga (30).
Mheshimiwa Spika, taarifa ya uchunguzi wa TALA inaonesha kuwa wanajeshi waliohusika hawakuwa wakifanya doria kama ilivyodaiwa na Mkuu wa Wilaya ya Ulanga isipokuwa walivamia na kupora mifugo, fedha na mali  ya wananchi na wakawa wanadai shilingi 10,000/= kwa kila kichwa cha mfugo ili wawaachie. Siku hiyohiyo walipora kiasi cha shilingi 205,000/= kutoka kwa watu wawili.
Mheshimiwa Spika, si nia ya Kambi ya Upinzani kuwasilisha Ripoti nzima ya tukio hili hapa, nia yetu ni kutaka kupeleka ujumbe kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa pamoja na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwamba vitendo kama hivi vinalivunjia Jeshi letu heshima kwa kiwango kikubwa sana mbele ya wananchi wa Tanzania na hata katika medani za kimataifa.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitishwa  sana na majibu ya kejeli yaliyokuwa yakitolewa na Mkuu wa Wilaya na Katibu Tawala wa Wilaya  ya Ulanga kwa wachunguzi wa TALA kwamba mauaji ya wananchi hao ni jambo la kawaida kama ajali nyingine. Mkuu wa Wilaya alilinganisha mauaji hayo na ajali ya gari iliyowapata wanamuziki wa FIVE STAR TAARAB iliyotokea Mikumi mwaka 2011.
Mheshimiwa Spika, majibu kama hayo licha ya kuendelea kuwaumiza kisaikolojia ndugu wa marehemu na majeruhi, ni ishara mbaya kwa wananchi kwamba Serikali haiwajali wananchi wake[1].
Mheshimiwa Spika, taarifa hizi za tukio la Jeshi la Wananchi kuwanyanyasa na kuwaua raia hazijengi taswira nzuri  kwa Jeshi letu na kwa  Raisi wa nchi ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Uslama.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inataka Serikali ielewe kwamba wananchi wameipa dhamana ya kumiliki nguvu za dola kwa madhumuni ya kuwalinda na kuwatetea. Kitendo cha nguvu hizi kutumika kuwaua na kuwanyanyasa wananchi ni matumizi mabaya ya dola na kwa maana hiyo Serikali sasa imekosa sifa ya kumiliki nguvu za dola.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kulieleza Bunge hili kama ina taarifa za matukio ya Askari wa Jeshi la Wananchi kuwapiga, kuwanyanyasa na kuwaua raia wanyonge wasio na silaha. Pili Serikali ieleze mbele ya Bunge hili hatua zilizochukuliwa kwa askari waliohusika na mauaji ya Ulanga.
5.0 Ahadi za Serikali na Utekelezaji wake katika Wizara ya Ulinzi na JKT Kuimarisha Kamandi ya Jeshi la Wanamaji
Mheshimiwa Spika, Serikali iliahidi kuimarisha kamandi ya Jeshi la Wanamaji ili kukabiliana na vitendo vya uharamia. Aidha, serikali iliahidi kununua meli za kivita kwa ajili ya ulinzi wa Exclusive Economic Zone. Majibu ya Serikali kuhusu ahadi hii ni kwamba wizara ipo katika hatua nzuri ya kuimarisha uwezo wa kulinda eneo la Exclusive Economic Zone bila kutaja mambo mahsusi iliyofanya. Pia kwenye ununuzi wa meli za kivita, Serikali inajibu kuwa upo mchakato ikiwa ni miaka miwili tangu ahadi hiyo itolewe.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaamini kwamba katika mambo ambayo hayahitaji kabisa propaganda za kisiasa ni pamoja na ulinzi na usalama wa nchi yetu. Ni aibu kwa Serikali kuahidi jambo muhimu hivi kwa ulinzi wa nchi na kutolitekeleza  kwa wakati. Ni aibu vilvile kwa Serikali kukiri kuwa na uwezo mdogo wa kufanya operesheni katika eneo la bahari kuu.
Mheshimiwa Spika, udhaifu katika kuimarisha kamandi hii ni dhahiri kumelisababishia taifa hasara kubwa kwani kumekuwa na wizi mkubwa wa rasilimali samaki. Meli iliyonaswa ikiiba samaki katika ukanda wetu wa bahari kuu, ni sehemu tu ya matukio ya kihalifu, ila matukio kama haya ya wizi wa rasilimali samaki yako mengi ila Serikali inashindwa kuyakabili kwa kukosa meli ya kivita kwa ajili ya kufanya doria katika eneo la bahari kuu.
Mheshimiwa Spika, kutokana na kamandi yetu ya Wanamaji kutokuwa na vifaa vya kutosha na vya kisasa, makampuni yanayotafuta mafuta na gesi kwenye ukanda wa bahari kuu yameamua kuajiri makampuni binafsi ya ulinzi yenye silaha nzito kutoka nje ya nchi, jambo ambalo ni la hatari kwa usalama wetu kama taifa.
Kambi ya Upinzani tunaitaka serikali kupiga marufuku mara moja makampuni ya nje kuingia na silaha nzito kwenye bahari yetu na tuimarishe kamandi ya Jeshi la wanamaji mara moja ili itumike kufanya shughuli hiyo ya kutoa ulinzi kwenye makampuni haya na hiyo itasaidia kuifanya bahari yetu kuwa salama.
6.0  Kuimarisha na Kukarabati Maghala ya Silaha
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2010/2011 Serikali iliahidi kuimarisha na kukarabati maghala makubwa na madogo ya kuhifadhi risasi, milipuko, mabomu na vifaa vingine. Maelezo ya Serikali katika ahadi hii ni kwamba JWTZ linaendelea na jitihada za kukarabati maghala hayo ingawa tatizo ni kwamba fedha zinazopatikana hazitoshelezi kukarabati na kuboresha maghala yote kwa wakati unaostahili.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitishwa sana na majibu mepesi ya Serikali kwa mambo mazito ya kiusalama kama haya. Wote tunakumbuka madhara makubwa yaliyotokana na milipuko ya mabomu katika maghala ya silaha huko Mbagala na hatimaye Gongo la Mboto, Dar es Salaam. Raia walipoteza maisha, wengine walipoteza mali na nyumba zao kuharibiwa vibaya na wengine kubaki na ulemavu wa kudumu katika viungo vyao. Madhara haya yaliwapata wanajeshi wetu vilevile.
Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya hatari namna hii, ni aibu kwa Serikali kusema kuwa haina fedha za kukarabati maghala ya Silaha lakini fedha za kulipa posho zisizo na tija hazikosekani. Hii ni ishara kuwa Serikali haijali usalama wa wanajeshi katika maghala hayo na raia walio jirani na maghala hayo.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasisitiza tena kwamba masuala yanayohusu ulinzi na usalama wa nchi yetu siyo ya mzaha hata kidogo. Serikali ihakikishe kwamba fedha za kutekeleza mikakati ya kiulinzi na usalama zinatolewa kwa wakati na mikakati hiyo itekelezwe kwa wakati uliopangwa.
7.0 Hali ya Usalama wa Mipaka ya Tanzania
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa iliyowasilishwa hapa Bungeni  mwezi Julai, 2011 ni kwamba mipaka ya nchi yetu ni shwari isipokuwa katika mpaka wa kusini ambapo tatizo la mpaka katika Ziwa Nyasa halijapatiwa ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Spika, kuendelea kuwa na tatizo katika Mpaka wa Ziwa Nyasa si dalili nzuri kwa usalama wa nchi yetu. Aidha, kuendelea kwa tatizo hili bila ufumbuzi wa mapema, kutadumaza uhusiano wetu na nchi jirani ya Malawi.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kutoa taarifa ya kiini cha mgogoro wa mpaka katika Ziwa Nyasa, na hatua ambazo zimechukuliwa hadi sasa kutatua tatizo hilo.
Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na malalamiko mengi toka kwa wananchi waishio maeneo ya mipakani mwa mkoa wa Kagera na nchi jirani kuwa wanavamiwa na makundi yanayosadikiwa kuwa ni askari wa majeshi na kuwaibia mali zao na mahali pengine kuingiza makundi makubwa ya mifugo katika mashamba yao.

Hivyo basi,  Mheshimiwa Spika, taarifa kuhusu usalama na ustawi wa mkoa wa Kagera unaonekana kuwa sio salama. Hili ni eneo ambalo Serikali imeshindwa kulitawala kiasi kwamba Umoja wa Mataifa unatambua kwamba hili ni eneo hatari kiusalama.

Mheshimiwa Spika, suala hili la kuvamiwa kwa wananchi na kutishiwa ni la muda mrefu na  Kamati mbalimbali za Kudumu za Bunge zimekwenda na kujionea hali halisi lakini kwa masikitiko makubwa ni kwamba hali ya usalama wa wananchi bado iko mashakani. Aidha, kwa sasa inakadiriwa kuna wahamiaji haramu wapatao 35,000 na mifugo yao zaidi ya 200,000 katika mistu ya hifadhi na maeneo mengine katika mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasisitiza kuwa mbali ya wahamiaji hao haramu, kuna tatizo kubwa katika ziwa Tanganyika ambapo kila mara wavuvi katika ziwa hilo wameporwa na wanajeshi wenye silaha nzito kutoka nchi jirani. Hivi, kwa matukio haya yote,  kama nchi tunapata wapi uthubutu wa kusema kuwa  mipaka yetu na wananchi wetu ni salama?

Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kupitia Jeshi letu kuweka ulinzi katika mipaka ya mkoa  wa Kagera  hasa kwenye Ziwa Victoria pamoja na kutoa ulinzi wa uhakika kwenye ziwa Tanganyika.
Aidha, tunaitaka serikali ilieleze Bunge hili ina mkakati gani wa makusudi wa kuwalinda wananchi wa Mkoa wa Kagera dhidi ya matishio kutoka kwa wahamiaji hawa haramu ambao wameishawaua au kuwajeruhi rai kadha licha ya kuwapora maeneo yao.
8.0  Jeshi la Kujenga Taifa
Mheshimiwa Spika, pamoja na umuhimu wa Jeshi la Kujenga Taifa katika kujenga ukakamavu, nidhamu na uzalendo miongoni mwa vijana wetu, jeshi hili pia limekuwa ni kiungo muhimu katika kukuza uchumi wa nchi kutokana na shughuli mbalimbali za uzalishaji mali.
Hata hivyo, kufuatia kusitishwa kwa programu ya kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa Sheria mwaka 1994 nidhamu miongoni mwa vijana imeshuka sana, uzalendo pia umeshuka na ndio maana vijana wengi wanashabikia vitu vya nje kuliko vya nchi yao; ukakamavu umeshuka na uvivu miongoni mwa vijana umeongezeka.
Mheshimiwa Spika, tayari hofu ya kuwa na Taifa la watu wazembe, wavivu, wasio wazalendo imeanza kujitokeza. Hata hivyo, hofu hii imeanza kutulizwa kidogo baada ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuhusu mapitio na mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2012/2013. Katika hotuba hiyo ukurasa wa 51, Waziri Mkuu alisema …. . “Jeshi la Kujenga Taifa limekamilisha ukarabati wa makambi 10 ya Jeshi la Kujenga Taifa yenye uwezo wa kuchukua vijana 20,000 kwa wakati mmoja. Kwa mwaka 2012/2013, jumla ya Vijana 5,000 wataanza tena kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa Sheria”.Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Spika, ni jambo jema kuwa Serikali imetambua umuhimu wa vijana kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mujibu wa sheria kwa vijana wetu waohitimu kidato cha sita. Kambi ya Upinzani inataka kufahamu kama zile sababu za kusitisha mafunzo ya JKT kwa vijana zimekwisha kabisa? Lengo la swali hili ni kuhakikisha kwamba utaratibu huu wa kujiunga na JKT unaoanza tena unakuwa ni endelevu na sio wa msimu. Pili, Kambi ya Upinzani inataka kujua vilevile kuwa Serikali ina mpango gani kwa wale vijana waliokosa mafunzo hayo tangu yalipositishwa?
8.1 Viwanda, utafiti na uendelezaji wa Teknolojia Jeshini
Mheshimiwa Spika, teknolojia ni jambo la msingi na muhimu sana katika kujenga jeshi la kisasa. Kabla ya kuwa na teknolojia ya kisasa suala la kwanza ni kuwa na rasilimali watu ambayo inao uwezo wa kubuni au kupokea na kuitumia teknolojia ya kisasa.
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri[2], alisema kuwa “……… ni kuendeleza utafiti na maendeleo ya teknolojia ya kijeshi katika viwanda vya kijeshi vya mashirika ya Mzinga na Nyumbu”, mwisho wa kunukuu. Kwa nukuu hiyo inaonyesha kuwa utafiti ni kwa ajili ya vifaa vya jeshi tu. Hii ni kutolitumia vyema Jeshi kwa manufaa ya wananchi na nchi kwa ujumla kama wenzetu wa mataifa yaliyoendelea wanavyotumia majeshi yao.
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Kambi ya Upinzani kwa mwaka wa fedha 2008/2009 iliongelea kuhusu umuhimu wa maendeleo ya sayansi na teknolojia[3]; naomba kunukuu: “Ili taasisi zetu za ulinzi zifanikiwe zinahitaji kuwa wazi, kuwa wavumbuzi na kukubali kubadilika na kuendana na maendeleo ya kisayansi na teknolojia. Mtaalamu wa fizikia Rutherford alinukuliwa akisema kwamba “we are short of money so we must think”. Wanajeshi wetu wafahamu kuwa tuna tatizo la rasilimali fedha, hivyo inawalazimu kuwa wavumbuzi na wabunifu zaidi kukabiliana na changamoto zilizopo hivyo tunahitaji vipaji binafsi. Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Spika, vipaji binafsi vya watendaji vinatafutwa toka ngazi za chini na kulelewa. Utaratibu huu ulikuwepo miaka ya nyuma, lakini kwa sasa nchi yetu imejikuta ikipoteza vijana wengi wenye vipaji kukimbilia nchi za nje na sasa wanafanya kazi huko. Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali ilieleze Bunge Jeshi letu lina mkakati gani wa kuibua vipaji na kuviendeleza ili kwa miaka ijayo tuwe na wanasayansi vijana wa kufanya tafiti sio tu kwenye nyanja za kijeshi bali pia kwenye nyanja za kilimo, madawa, mitambo, mifugo n.k
Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia katika Nyanja nzima za ulinzi na usalama, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kutenga ardhi ya kutosha kwa ajili ya Jeshi kufungua Makambi yanayoweza kuhamishika kulingana na mahitaji ya wakati huo kuliko kugawa ardhi kiholela kwa wageni ambao hadi sasa hatujui watu hawa wana nia gani na Taifa huko mbele.
8.2   Jeshi na Utekelezaji wa Kaulimbiu ya “Kilimo Kwanza”
Mheshimiwa Spika, ni jambo linalotia faraja kuona kwamba Jeshi letu la Kujenga Taifa linatekeleza kwa vitendo Kaulimbiu ya Kilimo Kwanza. Kwa mujibu wa Hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa katika Bunge la Bajeti, Julai 2011 ni kwamba katika mwaka 2010/2011 Jeshi la Kujenga Taifa lilima ekari 1,625 za kilimo cha mbegu bora kwa matarajio ya kuvuna tani 1,039 za mbegu mbalimbali.
Mheshimiwa Spika, pamoja mkakati huu mzuri, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali kuboresha mfumo huu usiwe wa kuzalisha mbegu peke yake bali pia kuwe na mikakati ya kujikita zaidi kwenye kilimo cha  mazao ya chakula ili kuinusuru nchi na majanga ya njaa na pia kudhibiti mifumuko ya bei inayotokana na ukosefu wa chakula nchini.  Kambi ya Upinzani inataka Serikali vilevile kutanua wigo wa shughuli za Jeshi la Kujenga Taifa kwa wananchi. Jeshi la Kujenga Taifa lishirikiane na Wananchi kwa maana ya kuwaelimisha namna ya kuendesha shughuli za kiuchumi na kijamii, mfano kilimo na utunzaji wa mazingira kwa ufanisi.
Mheshimiwa Spika, ili kutekeleza mkakati huu wa kuanzisha mahusiano ya Jeshi la Kujenga Taifa na Wananchi katika shughuli za uzalishaji mali, Kambi ya Upinzani inapendekeza kwamba wale watakaojiunga na Jeshi la Kujenga Taifa, wawe wanafanya mafunzo ya vitendo (internship) kwa wanachi, katika maeneo yatakayokuwa yamechaguliwa ikiwa ni sehemu ya ukamilisho wa mafunzo yao.
8.3 Utunzaji wa Mazingira
Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Taifa linashughulika pia na utunzaji wa mazingira ikiwa ni utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Mazingira. Hata hivyo, kwa mujibu wa Hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa aliyoitoa mwezi Julai, 2011, utunzaji wa mazingira umefanyika tu katika makambi na maeneo ya Jeshi kwa kupanda miti na kuhifadhi misitu katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inatoa pendekezo kwa Jeshi la Kujenga Taifa kuendesha OPERESHENI MAALUMU YA KUPANDA MITI NCHI NZIMA kwa awamu kwa kushirikiana na wananchi. Operesheni hii iendeshwe kwa utaratibu ule ule kwa watakaojiunga na JKT kufanya mafunzo ya vitendo wakishirikiana na wananchi katika kutunza mazingira.
Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo, Taifa hili litaepushwa na unyemelezi wa jangwa na athari za tabia nchi zinazotokana na uharibifu wa mazingira. Kambi ya Upinzani inataka mabadiliko katika Jeshi la Kujenga Taifa ili kazi zake ziwe ni za Kujenga Taifa kweli na sio kujenga na kuendeleza makambi ya Jeshi la Kujenga Taifa kama ilivyo sasa.
8.4   Kashfa ya Ufisadi kwa  Maafisa wa JKT
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Kambi ya Upinzani mwaka 2011/2012 tulizungumzia suala la SUMA JKT kuingia mkataba  wa ununuzi wa matrekta na mfanyabiashara ambaye alihusishwa na matukio ya ufisadi. Hata hivyo kwa mujibu wa taarifa rasmi za bunge za tarehe 13 Julai 2011 wakati waziri wa ulinzi anafanya majumuisho ya bajeti ya wizara yake alikanusha habari hizi. Alisema, na nanukuu:
 “…..hakuna ukweli hata kidogo kwamba SUMA JKT imeingia mkataba na mfanyabiashara, aliyemtaja Mheshimiwa Selasini”. Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, magazeti ya Uhuru, Nipashe, Jambo Leo ya tarehe 3 Julai 2012 yana taarifa kuhusu Maafisa wa Jeshi la Kujenga Taifa ambao pia ni wajumbe wa bodi ya SUMA-JKT kushtakiwa mahakamani kwa ufisadi wa matumizi mabaya ya madaraka na kuhamisha shilingi bilioni 3.8 kutoka katika akaunti ya Tanzania Korea Partnership (TAKOPA) kwenda kwenye akaunti ya SUMA-JKT.

Mheshimiwa Spika, taarifa hizi zinaashiria kuwa uongozi wa Jeshi la Kujenga Taifa una matatizo ya uadilifu. Sasa kama Jeshi lenye jukumu la kujenga Taifa hili linaongozwa na viongozi wa namna hii, Watanzania wategemee nini kwa vijana wanaojiunga na JKT? Kambi ya Upinzani inashauri kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afanye ukaguzi maalum katika Jeshi la kujenga Taifa na hususan SUMA- JKT. Pili, Serikali itoe maelezo katika bunge hili kuwa ina mpango gani wa dharura wa kusafisha taswira ya Jeshi la Kujenga Taifa ambayo imechafuka mbele ya jamii.



9.0 Maslahi ya Watumishi katika Jeshi la Wananchi na Jeshi la Kujenga Taifa
Mheshimiwa Spika, ni welewa wa kawaida kwamba ili mtu aweze kufanya kazi kwa ufanisi ni lazima apate mahitaji yake ya msingi yatakayomwezesha kuishi maisha ya staha. Kwa kuzingatia jambo hili, na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa kazi za majeshi yetu katika kulinda usalama na kujenga taifa letu, Kambi ya Upinzani inapendekeza maboresho ya maslahi ya watumishi katika jeshi yafanyike ili kuwapa motisha ili wafanye kazi kwa bidii zaidi.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali, kuandaa mazingira mazuri ambayo yatawasaidia wastaafu wa Jeshi kupata nafasi ya kufanya shughuli zitakazowapatia kipato cha ziada tofauti na mafao yao ya uzeeni. Kwa mfano Serikali iwakopeshe wanajeshi wastaafu fedha ili waanzishe vyuo vya mafunzo kwa vijana watakaotumika katika ulinzi shirikishi na ambao wataajiriwa katika makampuni binafsi ya ulinzi na kutoa huduma ya  ushauri wa kitaalamu (consultancy services)kwa makampuni binafsi ya ulinzi.


10.0.  Jeshi na Migogoro ya Ardhi na Fidia kwa Wananchi
Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sasa kumekuwa na migogoro mingi ya Ardhi baina ya wanajeshi na wananchi kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Migogoro hii imepelekea kuwepo kwa mvutano baina ya wananchi na jeshi letu kwa upande mmoja na viongozi wa wananchi kwa upande wa pili.
Mheshimiwa Spika, mifano ya migogoro hiyo ni  kama ile ya Ilemela , Tarime, Kunduchi na maeneo mengine mbalimbali ambayo yamekuwa yakilalamikiwa na wabunge kwa muda mrefu. Mara zote Serikali imekuwa ikitoa majibu kuwa itawalipa fidia wananchi ili waweze kuondoka na kuyapisha maeneo hayo kwa ajili ya Jeshi.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka huu wa fedha 2012/2013 zimeombwa kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kulipa fidia ya ardhi maeneo ya Mapinga, Shinyanga na Arusha.
Kambi ya upinzani inaona kuwa hakuna nia ya dhati ya kumaliza migogoro hii baina ya jeshi letu na wananchi kwani kiasi kilichotengwa ni kidogo mno kutosha kulipa fidia na hata maeneo yaliyotengewa fedha ni mawili tu. Tunaitaka serikali iwe na nia ya dhati ya kuwalipa wananchi fidia ili kumaliza migogoro hii ambayo inawafanya wananchi walichukie jeshi lao.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya Kambi ya Upinzani naomba kuwasilisha.
…………………………………….
Mch. Israel Yohana Natse (Mb)
Msemaji Mkuu Kambi ya Upinzani-Wizara ya Ulinzi ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
16.07.2012


[1] Chanzo:  REPORT ON TALA-MEDIA JOINT MISSION ON LAND RIGHTS FOR AGRO-PASTORALISTS AND FARMERS IN ULANGA DISTRICT (Gathering facts in response to the killings of 5 people done by Tanzania Peoples Defense Forces in Maguba area, Malinyi Ulanga 17th March, 2012)

[2] Hotuba ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa mwaka wa fedha 2008/2009 uk. 20
[3] Hotuba ya  Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani kwa mwaka wa fedha 2008/2009. Aya ya 14

No comments: