Friday, November 9, 2012

HOJA YENYEWE HII HAPA

HOJA BINAFSI YA KABWE ZUBERI ZITTO(MB) KUHUSU KULITAKA BUNGE  KUCHUNGUZA NA KUILEKEZA SERIKALI KUCHUKUA HATUA DHIDI YA RAIA WA WATANZANIA WALIOFICHA FEDHA NA MALI HARAMU NJE YA NCHI 

[Inatolewa chini ya Kanuni ya 54(3)]
Mbunge Zitto Kabwe
Mheshimiwa Spika,
KWA KUWAkumekuwa na uthibitisho kutoka Mamlaka za nchi ya Switzerland kwamba kuna raia wa Tanzania wanamiliki fedha za kigeni katika Benki nchini na kwamba kuna kanuni na taratibu za nchi zinazoendesha na kuongoza ufunguaji wa akaunti za fedha za kigeni nje ya Tanzania kwa Watanzania wakazi (residents). Na kwamba kitendo kilichofanywa na wahusika kuweka mabilioni ya fedha kwenye nchi za nje kinaweza kuwa ni kinyume na sheria ya FOREIGN EXCHANGE ACT, 1992”

NA KWA KUWA sheria hiyo kifungu cha (10) cha Sheria ya Fedha za kigeni kinazuia utoroshaji wa fedha za kitanzania na isipokuwa kwa kibali cha Gavana wa Benki Kuu tu, hakuna mtu yeyote atakaye ruhusiwa  kusafirisha fedha nje ya Tanzania. 
Na kinaeleza kuwa kwa msafiri anayekwenda nje ya nchi hatoruhusiwa kuondoa na kiasi cha shilingi ambazo zinazidi dola za kimarekani hamsini. Vile vile kwa mujibu wa Sheria hiyo kifungu cha 6 na 7 na waraka uliotolewa na Gavana wa Benki Kuu kwamba Mtanzania yeyote mwenye kutaka kufungua akaunti kwenye mabenki nje ya Tanzania lazima apate kibali cha Gavana.

NA KWA KUWA masharti hayo ya sheria yanaweza kuwa yamekiukwa na wahusika kwa kuhifadhi fedha za kigeni katika mabenki ya nje,

NA KWA KUWA ukiukwaji huo ni dhahiri kuwa fedha zilizowekwa kwenye mabenki ya nje kwa kiasi kikubwa ni fedha ambazo hazikupatika kwa njia za halali na kwamba kuna uwezekano wa ukwepaji mkubwa wa kodi,

NA KWA KUWA, nchi yetu imekuwa katika matatizo makubwa ya fedha za kigeni, jambo ambalo limepelekea nchi kushusha thamani ya shilingi ili kukabiliana na gharama za manunuzi ya bidhaa nje ya nchi,

NA KWA HIYO BASI, ninaliomba Bunge hili liazimie:
1.    Kwamba Bunge lako tukufu liunde Kamati Teule kuchunguza Raia wa Tanzania wenye kumiliki fedha za kigeni na mali nje ya Tanzania. Kamati Teule hiyo ifanye kazi zifuatazo:
-         Kuchunguza mfumo mzima wa utoroshaji wa fedha na kufichwa nje ya nchi,
-         kuchunguza na kupembenua mali na fedha haramu dhidi ya halali zinazomilikiwa na raia wa Tanzania katika taasisi za kifedha nje ya Tanzania,
-         kuchunguza utaratibu mzima wa kugawa vitalu vya utafutaji mafuta na gesi kati ya mwaka 2003 mpaka 2008,
-         kuchunguza mtiririko mzima wa utoroshaji wa fedha kutoka Benki Kuu ya Tanzania kupitia Kampuni ya Meremeta (pia Triannex pty ya Afrika Kusini na Deep Green Finance ltd) na kupendekeza hatua za kuchukua dhidi ya wahusika wote wa utoroshaji wa fedha kwenda nje,
-         kuchunguza umiliki wa wa watanzania kwenye kampuni zote zenye mikataba ya utafutaji wa Mafuta na Gesi hapa nchini na namna umiliki huo umekuwa ukibadilika, mapato (proceeds) zilizotokana na mabadiliko hayo ya umiliki na kama kodi stahili zimekuwa zikilipwa kutokana na kubadilika kwa umiliki huo,
-         kuchunguza kwa kina mali za Watanzania wote waliowahi kushika nafasi za Uwaziri Mkuu kati ya mwaka 2003 mpaka 2010, waliowahi kushika nafasi za Uwaziri wa Nishati na Madini, Uwaziri wa Ulinzi, Ukuu wa Majeshi, Ukatibu Mkuu wa wizara ya Nishati na Madini, Ukatibu Mkuu wa Wizara ya Ulinzi, Uanesheria Mkuu wa Serikali, Ukamishna wa Nishati, Ukurugenzi Mkuu wa TPDC, Uenyekiti na Ujumbe wa Bodi wa TPDC katika ya mwaka 2003 mpaka 2010.
2.    Kwamba Serikali ilete muswada wa Sheria Bungeni ifikapo Mkutano wa 11 wa Bunge kwamba itakuwa ni marufuku kwa Kiongozi yeyote wa Umma au mume au mke wake au watoto wake kuwa na akaunti katika mabenki nje ya nchi isipokuwa kwa sababu maalumu na kwa kibali rasmi kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

3.    Kwamba Serikali iwasiliane na Benki ya Dunia ili kupitia Kitengo cha Assets Recovery Unit mabilioni ya Fedha na mali zisizoondosheka zinazomilikiwa na Watanzania katika mabenki ya nchini Switzerland, Dubai, Mauritius na visiwa na maeneo mengine yote ambapo hufichwa fedha na Mali ili kukwepa kodi  na kwamba mali hizo na mabilioni hayo yaliyopatikana kiharamu yarudishwe nchini mara moja
4.    Kwamba katika muswada tajwa hapo juu, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania aimarishiwe mamlaka ya kutoa kibali kwa Mtanzania yeyote anayetaka kufungua akaunti ya Benki nje ya nchi na kwamba kila mwaka Gavana atatangaza kwenye Gazeti la Serikali na magazeti yanayosomwa na wananchi wengi orodha ya Watanzania walioomba na walioruhusiwa kuwa na akaunti ya Benki nje ya Tanzania.
5.    Kwamba Watanzania wote wenye akaunti za fedha nje waeleze wamezipataje na TAKUKURU wachukue hatua za kisheria dhidi ya watu wote wenye kumiliki fedha na mali kinyume na mapato yao halali.
6.    Kwamba Serikali, katika mkutano wa Bunge wa 11 na baada ya Taarifa ya Kamati Teule ya Bunge kuhusu Raia wa Tanzania wenye kumiliki fedha za kigeni kwneye mabenki na mali nje ya Tanzania ilete taarifa ya hatua ilizochukua ili kuziba mianya ya utoroshaji wa fedha nje ya Tanzania.
7.    Kwamba Serikali katika Bajeti ya mwaka 2013/14 itaanzisha kodi maalumu ‘financial transaction tax’ ya angalau asilimia 0.5 ya thamani ya ‘transaction’ ili kuweza kuwa na rekodi za uhakika za fedha ndani na zinazotoka nje ya nchi.


Mheshimiwa Spika,

Naomba kutoa hoja,
…………………….
KABWE ZUBERI ZITTO(MB)
JIMBO LA UCHAGUZI-KIGOMA KASKAZINI
08.11.2012

UKURASA UNAOFUATA UNAYO HOJA HIYO TANGU MWANZO, HII HAPA NI SEHEMU YA HOJA HIYO

No comments: