Kampuni kubwa zaidi duniani ya madini ya Platinum, Anglo American Platinum, imewaachisha kazi wachimba migodi 12,000 waliokuwa wanagoma kudai nyongeza ya mishahara.
Kampuni hiyo, Amplats, ilisema kuwa mgomo haramu wa wiki tatu uliofanywa na takriban wachimba migodi 28,000 mjini Rustenburg, uliiletea hasara ya dola milioni 82.3.
Ikieleza sababu ya kuchukua hatua hiyo, Amplats, ilidokeza kuwa, wachimba migodi walikosa kuhudhuria vikao vya kinidhamu na ndiyo maana wakaachishwa kazi.Sekta ya madini nchini Afrika Kusini, imekumbwa na migomo ya wachimba migodi na hata kukatokea maafa baada ya polisi kuwapiga risasi zaidi ya wachimba migodi 30, waliokuwa wanagoma kutaka waongezwe mishahara.
>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>
Idadi ya malori yaliyokwama kwenye mpaka wa Zambia na DRC yafikia karibu 1000
Gazeti la Times of Zambia limesema idadi ya malori yaliyokwama katika mpaka wa Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC imefikia karibu 1000 huku madereva wakiwa wanaendelea kususia kuingia nchini DRC.
Madereva wa malori kutoka nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC walianza kususia kuingia DRC Jumatatu kutokana na usumbufu uliofanywa na maofisa wa nchi hiyo, na kusababisha malori 600 kukwama kwenye mpaka wa Kasumbalesa, upande wa Zambia.
Lakini idadi ya malori imeongezeka na kufikia karibu 1000, ambapo madereva wameshikilia kuwa hawataingia DRC hadi madai yao yatakapotimizwa na serikali ya nchi hiyo. Madereva hao wanataka kuhakikishiwa kimaandishi na mamlaka za Kongo, kwamba zitashughulikia usumbufu huo.
>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>>
Baraza la usalama lalaani mashambulizi ya makombora kwenye mipaka kati ya Syria na Uturuki
Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa jana tarehe 4 lilitoa taarifa likilaani vikali tukio la mashambulizi ya makombora lililotokea kwenye maeneo ya mpaka kati ya Syria na Uturuki, pia limezitaka pande mbalimbali zijizuie.Baraza hilo limezitaka pande husika ziache kufanya vitendo vya kukiuka sheria ya kimataifa, na kutorejea tena kufanya vitendo hivyo. Vilevile baraza hilo limeitaka serikali ya Syria iheshimu mamlaka na ukamilifu wa ardhi wa nchi jirani.
Hivi sasa mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa nchi za kiarabu anayeshughulikia suala la Syria Bw. Lakhdar Brahimi anaendelea kuwasiliana na maofisa wa Uturuki na Syria, ili kupunguza hali ya wasiwasi.
Mjumbe wa Syria kwenye Umoja wa Mataifa siku hiyo alisema, serikali ya Syria inasikitishwa na vifo vya raia wa Uturuki, na Syria inafanya uchunguzi wa tukio hilo.
Jumuia ya NATO, Marekani na Ufaransa zimelaani tukio hilo, huku Russia na China zikizitaka pande husika zijizuie, na kuepusha vitendo vyovyote vitakavyofanya hali ya wasiwasi izidi kuwa mbaya.

No comments:
Post a Comment