Sunday, June 10, 2012

JK - ATUMA SALAMU ZA RAMBI RAMBI KUFUATILIA KIFO CHA MUASISI WA CHADEMA BOB MAKANI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameitumia  familia ya Mzee Bob N. Makani, salamu za rambirambi kuomboleza kifo cha Mzee huyo kilichotokea usiku wa kuamkia jana katika Hospitali ya Aga Khan ya Dar es Salaam.

Katika salamu zake za rambirambi, Rais Kikwete amesema kuwa amehuzunishwa na kusikitishwa na habari za kifo cha Mzee Makani ambaye alilitumikia taifa la Tanzania kwa uadilifu na uzalendo katika nafasi mbali mbali alizozishikilia katika maisha yake ikiwamo ile ya Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania.

“Nimepokea kwa huzuni na masikitiko habari za kifo cha Mzee Makani ambaye nimejulishwa kuwa aliaga dunia usiku wa kuamkia jana katika Hospitali ya Aga Khan mjini Dar es Salaam. Nilimfahamu Mzee Makani vizuri wakati wa uhai wake. Alikuwa Mzalendo na mtumishi mwadilifu wa umma, sifa ambazo alizithibitisha katika nafasi zote alizozishikilia katika utumishi wa umma ama kwenye siasa.”

Nawatumieni salamu za rambirambi za dhati ya moyo wangu, nikiwajulisheni kuwa niko nanyi katika msiba huu mkubwa ambao umewaondolea mpendwa wenu, baba yenu, babu yenu na mhimili wa familia yenu. Napenda mjue kuwa msiba wenu ni msiba wangu. Naelewa machungu yenu katika kipindi hiki, lakini nawaombeeni subira na uvumilivu kwa sababu yote ni mapenzi ya Mungu. 

Naungana nanyi katika kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, ailaze pema peponi roho ya Marehemu Makani. Amen.”

No comments: