UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi
hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kuwepo hapa leo kuwasilisha maoni ya Kambi ya Upinzani kuhusu Wizara
ya Ardhi, Nyumba Na Maendeleo ya
Makazi .
Mheshimiwa
Spika, pia nikushukuru
wewe kwa kuniruhusu kutoa maoni
ya Kambi ya Upinzani kuhusu
Wizara hii kwa mujibu wa Kanuni
ya 99 kanuni ndogo ya (7) , ya
Kanuni za Bunge Toleo la Mwaka 2007.
Mheshimiwa
Spika, pili
ningependa kutoa shukrani zangu za
dhati kwa Chama Cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA) na wananchi wa Jimbo la Kawe ( wapiga kura wangu) kwa
imani yao kwangu, makamanda wote
(vijana, wazee na akina mama wa vyama vyote)
kwa kuendelea kuniunga mkono katika kuhakikisha Jimbo letu linapata
huduma zote za msingi zinapatikana
katika viwango stahili. Ahadi yangu kwenu ni kuwatumikia kwa uwezo wangu wote
kwa kadiri Mwenyezi Mungu atakavyoniwezesha!
Mheshimiwa
Spika, napenda pia kutoa
shukrani za dhati kwa CHADEMA kikiwa chini ya Mtendaji wake mkuu (KATIBU
MKUU-TAIFA), Mhe. Wilbroad Peter Slaa. Hakika
kila Mtanzania anaona kazi unayoifanya ya kuhakikisha chama chetu kina
kuwa juu na Watanzania wote wanatuunga mkono. Mungu akupe uhai, naamini ipo
siku tutaifikia Nchi ya Ahadi!
Mheshimiwa Spika, sina budi kumshukuru Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Mhe. Freeman
Aikaeli Mbowe, kwa kuniamini na kuniteua
tena kuwa Msemaji Mkuu wa Kambi ya
Upinzani katika Wizara hii. Shukrani pia
ziende kwa wasaidizi wa Kiongozi wa
Kambi, Kabwe Zitto (Naibu Kiongozi wa Kambi) na Tundu Lissu (Mnadhimu wa Kambi)
kwa kutuongoza vyema katika shughuli hii ngumu ya kuwatetea wanyonge. Shukrani
pia ziwafikie wabunge wenzangu wote wa Kambi kwa ushirikiano wao kwangu.
Mheshimiwa Spika, kipekee niishukuru sana familia
yangu yote, wazazi wangu Prof. James Salehe Mdee na Theresia Kisenga Ngowi kwa
upendo wao na kwa upekee nimshukuru kaka yangu Joseph James Mdee,kwa msaada na
ushauri mkubwa katika kuhakikisha natimiza majukumu yangu ya kibunge ndani na
nje ya Bunge. Asanteni sana!!!
HOJA ZA
KAMBI YA UPINZANI 2011/12
Mheshimiwa Spika, kufuatia hotuba ya Kambi ya Upinzani
Bungeni ya mwaka 2011/12 Kambi ya upinzani inatambua hatua zilizochukuliwa na
serikali katika hoja kadhaa ambazo
ziliwasilishwa kwake hususan suala la ada ya ukodishwaji wa mashamba na vitalu
ambapo serikali ilikuwa inatoza shilingi 220 tu kwa eka. Kauli ya serikali
kupitia Naibu Waziri wa ardhi wakati akichangia hotuba ya mapitio na mwelekeo
wa kazi za serikali na
makadirio ya matumizi ya fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu 2012/2013 imeonyesha
nia ya serikali kuongeza ada husika ili kuiongezea serikali mapato.
Kambi ya Upinzani inatambua pia hatua ambazo
serikali imeahidi kuzichukua katika mwaka huu wa fedha 2012/13 kwa kutenga
fedha za fidia kwa wananchi wa Kurasini Mabwawani. Serikali imeeleza kwamba
fidia zitalipwa kwa viwango vipya kuendana na thamani ya soko!
Halikadhalika, Kambi ya Upinzani
inatambua hatua zitakazochukuliwa na serikali kuhusiana na mwekezaji Agrisol ,
ili kuiepusha nchi kuingia kwenye
mkataba mbovu usiozingatia maslahi na sheria za nchi. Kambi ya upinzani
imefarijika na Kauli ya Waziri Mkuu wakati akihitimisha hotuba yake ya bajeti
ambapo, pamoja na mambo mengine alitamka kwamba mchakato wa Agrisol haujaanza, hawajaingia
makubaliano/mkataba ”wowote” na kwamba
mchakato ukianza ndipo wataingia kwenye mambo ya msingi waone wanapangiana vipi, uwiano utakuwaje na kwamba
halmashauri imiliki kiasi gani cha hisa!
Mheshimiwa Spika, rai ya Kambi ya Upinzani ni
kwa serikali kusitisha mpango wake wa
kuligawa eneo la Mishamo na Katumba
lenye ukubwa wa zaidi ya hekta
325,000 au ekari 760,728 kwa AGRISOL. Kuna taarifa kwamba tayari serikali
ilishaligawa eneo la Lugufu lenye ukubwa
wa hekta 10,000 kwa AGRISOL (kwa kuwa mikataba
inaendeshwa kwa usiri mkubwa.) Ni imani yangu Serikali itatupa jibu juu ya mustakabali wa Lugufu.
Mheshimiwa Spika, wakati serikali
ikitafakari, ni muhimu Bunge hili tukufu likaelewa kwamba aliyekuwa mshirika
muhimu wa Agrisol IOWA State University College of Agriculture aliyekuwa
mhimili muhimu wa mwekezaji huyu hasa katika kuwasaidia wakulima wadogo wadogo
kama ilivyoainishwa katika kipengele cha
4.7 cha MoU baina Halmashauri
ya wilaya ya Mpanda na AGRISOL ENERGY TANZANIA LIMITED alijitoa
baada ya kugundua kwamba mwekezaji huyu hana dhamira ya kuisaidia nchi na wakulima
wadogo zaidi ya kujinufaisha kibiashara.
Mheshimiwa Spika, kwa maelezo ya IOWA State
University College of Agriculture, ilijitoa baada ya kugundua ilitumiwa na
mmiliki wa AGRISOL bwana Bruce Rastetter
ili aweze kupata uhalali wa kukubalika
kirahisi kama mwekezaji mahiri! Ukweli ni kwamba nia ya mwekezaji huyu haikuwa kuisaidia nchi bali kuendeleza mashamba makubwa ya zao
mojamoja,.. matumizi ya viwango vikubwa vya kemikali na pia kuomba mabadiliko
katika kanuni za kitaifa za usalama wa kibiolojia ili mazao yenye viinitete
yaweze kupandwa.
Mheshimiwa
Spika, madhara ya GMO ni
makubwa sana, moja kubwa ni kufifisha kabisa matumizi ya mbegu za asili. Mwekezaji akizitumia kwenye eneo lake, madhara
yanasambaa pia kwa mashamba ya jirani, inajenga utegemezi wa wakulima kununua
mbegu kutoka kwa wakulima wakubwa. Mbali na utegemezi wa mbegu, GMO zina
madhara makubwa sana kiafya. Tafiti zimeonyesha kwamba nchi zilizoendelea ziko
katika vita kali sana za kuzuia matumizi ya GMO lakini sisi tunayapokea
makampuni makubwa kwa misamaha lukuki ya kodi, tukiamini tunaalika wawekezaji
waje kuijenga nchi, kumbe wanakuja kutengeneza taifa la utegemezi na lenye
maradhi lukuki.
Mheshimiwa
Spika, ni muhimu ikaeleweka
kwamba katika wilaya ya Mpanda ardhi ambayo iko wazi kwa matumizi ya binadamu (arable
land) ni 19% tu ya eneo lote! Nyingine iliyobaki ni hifadhi za taifa:
i)
18% hifadhi
ya wanyama,
ii)
59% hifadhi ya misitu
iii)
4% hifadhi ya maji.
Mheshimiwa
Spika,badala ya kila kitu kuwategemea mabeberu, inawezekana kabisa serikali ikawekeza katika eneo husika. Taarifa
zinaonyesha kwamba AGRISOL walitarajia kuwekeza $100 milioni (shilingi bilioni 150) katika kipindi cha miaka 10,
kwa matarajio ya kupata faida ya $272 milioni
(shilingi bilioni 408) ndani ya mwaka mmoja baada ya uwekezaji huo kwa kulima
hekta 200,000 tu za mahindi, kiasi ambacho
kinalingana kama sio kuzidi bajeti ya Wizara ya Kilimo!
Mheshimiwa Spika, kama Agrisol wangepata/watapata
hadhi ya mwekezaji wa kimkakati,(stratergic
investor). Wangepata/watapata pia msamaha wa kodi ya shirika (corporate tax) ambayo ni 30% ya shilingi bilioni 408 (ambayo
ni bilioni 122)! Hivi kweli serikali makini, mbali ya kuwa na vivutio vya
utalii vilivyosheheni, na hivyo kuwa
nchi ya nne ya uzalishaji wa dhahabu Afrika, nchi pekee yenye madini tofauti
tofauti zaidi ya 15 na kwa upekee ni madini ya Tanzanite, tuna urani ya kutosha, hivi karibuni tumegundua gesi yenye thamani
ya tsh trilioni 626.7, tuna tani milioni
86 za makaa ya mawe, tuna kila dalili ya kupata mafuta n.k inashindwa kuwekeza kwa
faida ya nchi na wananchi wake? Tunawezaje kuokoa kizazi cha vijana waliogeuka
wazururaji kwa sababu serikali yao haijawapa fursa?
Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka 2011/2012,
Kambi ya Upinzani ilielezea kwa kina matatizo sugu ya migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini ambayo imekithiri kufikia hatua ya uvunjifu
wa amani kunakopelekea umwagaji damu na
wakati mwingine vifo kutokea. Mwaka mmoja umepita bado hakuna hatua dhahiri zilizochukuliwa na
serikali hususan kuhusu:-
i)
Mgogoro wa ardhi unaowahusisha wakulima wa kijiji cha Nzasa, ambapo Wizara ya Maliasili na Utalii wanataka
kuwaondoa wananchi katika ardhi yao
halali kwa madai kwamba wanaishi ndani ya hifadhi ya Msitu wa Kazimzumbwi.
ii)
Mustakabali wa maeneo ya yaliyokuwa mashamba ya
Ngano, Hanang (Hanang Wheat Complex (HWC) na Dakawa Ranch.
iii)
Tatizo la ukodishwaji wa mashamba unaofanywa na
wawekezaji dhidi ya wananchi wenyeji.
Hususan shamba la mpunga la Mbarali na Kapunga,
yote yakiwa wilaya ya Mbarali na
mwekezaji RAI group anayemiliki mashamba ya Setchet, Murjala na Gidagamowd ambaye alikuwa
anawakodisha wananchi $10 kwa ekari.
Kambi ya Upinzani ina taarifa za kuendelea kwa
ukodishaji wa mashamba unaofanywa na wawekezaji. Shamba la hekta 1 hukodishwa
kwa shilingi laki moja mpaka laki moja na nusu
katika mashamba ya Kapunga na Mbarali.
Hoja ya Kambi ya Upinzani imethibitishwa pia na timu ya
wataalam wa Consolidated Holding
Corporation (CHC) katika taarifa yao ya ufuatiliaji wa mashamba
na viwanda vilivyobinafsishwa[1] ambayo inabainisha
kwamba katika shamba la Mbarali Rice Farm mwekezaji analima sehemu ya
shamba na sehemu nyingine ya shamba anakodisha kwa wananchi kwa utaratibu
maalum.
iv)
Kambi ya Upinzani inataka kujua mustakabali wa
kijiji cha Kapunga, kilichopo wilaya ya Mbarali ambacho kiliuzwa kwa mwekezaji! Mkataba wa mauzo na Hati miliki ya shamba (certificate of
title) zinaonyesha kuwa shamba lina
ukubwa wa hekta 7,370. Wanakijiji wanadai kuwa shamba linatakiwa kuwa na ukubwa wa hekta 5,500 kulingana na barua ya maombi ya ardhi
kutoka kwa NAFCO na muhtasari wa mkutano
wa kijiji ulioidhinisha utoaji wa eneo
husika.
v)
Mashamba
ya Gawal na Warret yaliyopo Hanang yalitakiwa kurejeshwa kwa wananchi lakini hayajarejeshwa.
vi)
Mgogoro wa ardhi baina ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) na wananchi wa Bukanga na Buhare (Mgaranjab) Musoma Mjini.
vii)
Mgogoro unaohusu shamba namba 299 (iliyokuwa
NARCO Ranches) lenye ukubwa wa hekta
49,981. Halmashauri ya wilaya ya Mvomero. Mgogoro huu uliwahusisha vigogo
wakubwa wastaafu wa Chama cha siasa na serikali.
viii)
Mgogoro
baina ya Simba Motors na wanakijiji
wa Mapinga, kitongoji cha
Undindivu, wilaya ya Bagamoyo.
ix)
Mgogoro baina ya wakulima na wafugaji wa jamii ya Wamasai katika eneo la vijiji vya Izava
(Chamwino) na Chitengo (Kongwa).
x)
Uvamizi wa
maeneo ya wazi Mkoa wa Dar es salaam; viwanja vingapi vimerejeshwa kwa
matumizi ya umma? Na viwanja vingapi bado vipo mikononi mwa wavamizi?
MATATIZO YA TATHMINI NA MALIPO YA FIDIA
Mheshimiwa Spika, imekuwa ni jambo la kawaida
sana kwa zoezi la fidia kuendeshwa kihenyeji na pasipo kuzingatia sheria na
taratibu tulizojiwekea! Na hata wananchi wakilalamika serikali inaendelea na
miradi! Kambi ya Upinzani inataka majibu ya hoja zifuatazo ambazo licha ya
kuzungumzwa katika bajeti ya 2011/12 bado serikali haijazipatia majibu:
a)
Hatma ya wanakijiji wa kijiji cha Mabwepande
ambao miaka mitano iliyopita serikali
ilifanya tathmini na kuwaagiza wasifanye
maendeleo yoyote ili kupisha ujenzi wa chuo cha IFM. Pia baada ya
mafuriko makubwa yaliyolikumbwa jiji la Dar es salaam maeneo yao yalichukuliwa
na serikali kwa ajili ya kugawa viwanja kwa waathirika! Mpaka sasa hakuna fidia
yoyote iliyolipwa!
b)
Hatma ya Wananchi wa Kigamboni.
c)
Hatma ya wananchi 1600 wa wilaya ya Mbarali
waliotakiwa kuondoka kupisha upanuzi wa
mbuga ya Taifa ya Ruaha.
UTEKELEZAJI WA BAJETI 2011/12
Mheshimiwa Spika, mpango wa Taifa[2]
umeainisha wazi kwamba, pamoja na mambo mengine kufanikiwa kwake kunategemeana sana na mipango
bora ya matumizi ya ardhi. Na chombo pekee cha kuweza kufanikisha hili ni Wizara ya Ardhi kupitia taasisi yake ya Tume
ya Taifa ya Mipango. Kati ya majukumu ya Tume ni:-
i)
Kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya
vijiji.
ii)
Utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Matumizi ya Ardhi kwa kutekeleza programu za kilimo, mifugo na maji kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo, Maji na Kilimo.
iii)
Kusaidia
kupatikana kwa ardhi kwa ajili ya
utekelezaji wa KILIMO KWANZA.
iv)
Kufanya utafiti katika masuala yanayohusiana na ardhi hasa katika
maeneo yenye migogoro, uhamiaji mijini kutoka vijijini, ushirikishwaji wananchi katika kuendeleza ardhi mijini,
viwango vya matumizi ardhi mijini na vijijini.
v)
Kufuatilia
na kutathmini mipango ya matumizi
ya ardhi iliyokwisha andaliwa na katika
maeneo yenye migogoro sugu.
Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba majukumu yao
yangekuwa yanachukuliwa kwa uzito unaostahili, leo tungekuwa hatuzungumzii hoja
za migogoro ya ardhi ambayo kwa sasa ni tishio la amani ya nchi, bali mafanikio
ya matumizi endelevu ya rasilimali kubwa ya ardhi tuliyobarikiwa na mwenyezi
Mungu!
KUPUUZWA KWA MIRADI YA MAENDELEO
Mheshimiwa Spika, licha ya umuhimu na ukubwa
wa majukumu yake, Wizara ya Ardhi ni kati ya wizara ambazo zinapewa fedha ndogo
sana za kutekeleza miradi ya maendeleo! Na mbaya zaidi, licha ya ufinyu wa
fedha, fedha zimekuwa hazipelekwi zote!
Mwaka wa fedha 2010/11 Wizara
iliidhinishiwa jumla ya shilingi 22,265,078,000/- kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hadi mwaka
unaisha, wizara ilipokea jumla ya shilingi 4,673,383,000/- tu! Ambapo fedha zilizotumika kutekeleza miradi ya
maendeleo ni shilingi 3,931,581,086/- zilitumika kutekeleza miradi ya maendeleo! [3]
Hali kadhalika, katika mwaka
wa fedha 2011/12, wizara iliidhinishiwa jumla ya shilingi 22,010,437,000/ kwa ajili ya miradi ya
maendeleo . Hadi Mei 2012, Wizara ilipokea shilingi 3,663,685,463.96/- tu kwa jili ya miradi ya maendeleo!
Mheshimiwa spika, uzembe wa aina hii hauwezi
kuvumilika! Kambi ya Upinzani inaitaka serikali ilieleze Bunge lako tukufu, ni
kwa nini kwa miaka miwili mfululizo fedha za maendeleo zimekuwa hazitolewi kama zilivyopangwa!
Sambamba na hilo, ni miradi mingapi imekwama kutokana na upungufu huo?
KUPUUZWA KWA MAELEKEZO YA WAZIRI MKUU
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia changamoto za
kimapato zinazoikabili Wizara ya Ardhi,
serikali kupitia kauli ya Waziri Mkuu iliridhia kuipatia wizara kibali cha kubakia na makusanyo yao asilimia
100. Naomba kumnukuu:
’Mheshimiwa
Naibu Spika,lakini nasema hivi, jana tukiwa kwenye Cabinet
tumemuidhinishia huyu mama kwamba wewe mama ile fedha yote ambayo utakuwa unakusanya kutokana na
shughuli zako za ardhi baki nayo yote,
chukua yote ili ikusaidie wewe katika
uendeshaji wa wizara hiyo.Kwa hiyo tunatambua
changamoto alizonazo na naamini
tutamsaidia vizuri sana na najua ataweza’ Mwisho wa kunukuu.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2011/12, hadi
Mei 2012 , Wizara ilikusanya jumla ya shilingi bilioni 16. Kinyume na maelekezo ya Waziri Mkuu, wizara ilipokea kiasi cha bilioni 9.4 tu, sawa na
asilimia 59 ya kilichokusanywa!
Kutokana na upungufu huo wizara
ilishindwa kuongeza gawio la fedha za retention
kwa Halmashauri mpaka kufikia 30% badala ya gawio la sasa la 20%! Kambi ya Upinzani
inaitaka serikali itoe maelezo juu ya mustakabali wa kiasi cha retention
ambacho bado hakijapelekwa Wizarani!
MATUMIZI YANAYOHITAJI MAELEZO
MISHAHARA
Mheshimiwa Spika, imekuwa ni utaratibu wa Bunge lako tukufu kupitisha mafungu
mbali mbali kama yalivyoombwa na wizara
na idara mbalimbali za serikali. Tafsiri ikiwa kila wizara au idara ya serikali
ina ufahamu wa makadirio ya fedha ambazo ina tarajia kutumia katika fungu
husika. Kwa miaka miwili mfululizo
wizara ya ardhi imekuwa ikitumia fungu la mshahara kuliko kiasi
kilichoidhinishwa na Bunge.
Katika mwaka wa fedha
2010/11, wizara iliidhinishiwa jumla ya shilingi 6,423,295,000/- kwa ajili ya
mishahara. Lakini katika
kipindi cha Julai 2010 hadi Mei 2011
kiasi cha shilingi 8,499,539,334/- zilitumika kulipa mishahara. Hali kadhalika katika mwaka wa fedha 2011/12 wizara iliidhinishiwa shilingi 7,531,409,000/-
kwa ajili ya matumizi ya mishahara. Hadi Mei 2012 kiasi cha shilingi 9,765,774,300/- zilitumika kulipa mishahara! Kambi ya Upinzani
inaitaka serikali itoe maelezo, hiyo tofauti
(ya zaidi ya shilingi bilioni mbili) ya kiasi kilichoidhinishwa na
Bunge na kiasi kilichotumiwa na wizara
kwa miaka miwili mfululizo imetokana na
nini!
MIPAKA YA KIMATAIFA
Mheshimiwa
Spika, Serikali ilikuwa katika mchakato wa kuandaa andiko la kuomba eneo la nyongeza nje ya
ukanda wa kiuchumi baharini . Andiko hili liliwasilishwa Umoja wa Mataifa tarehe 18 Januari 2012. Kwa mwaka wa fedha
2010/11 na 2011/12 kiasi cha shilingi
431,572,872/- na 171,920,854.59/-
zilitumika kuandaa andiko husika! Kambi ya Upinzani inaitaka serikali
kutoa mchanganuo wa matumizi husika na kuainisha ni kwa namna gani ANDIKO
limeweza kuigharimu serikali zaidi ya shilingi milioni mia sita!
MASHAMBA YALIYOBINAFSISHWA AMBAYO HAYAJAENDELEZWA
Mheshimiwa Spika, wakati akihitimisha bajeti ya ardhi mwaka
jana, Waziri wa ardhi aliliahidi bunge lako tukufu kwamba baada ya bunge la
bajeti wizara ingekwenda kufanya ukaguzi
huru wa nani ametelekeza mashamba. Alisisitiza kwamba wawekezaji wote waliotelekeza mashamba the honeymoon is over.[4]
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka kupata idadi ya mashamba yaliyokaguliwa na wizara na mahali yalipo
toka ahadi husika ilipotolewa na ni
hatua gani ambazo zimeshachukuliwa na
serikali dhidi ya wawekezaji husika.
Mheshimiwa
Spika, wakati Kambi ya Upinzani
ikisubiri taarifa toka kwa waziri wa ardhi juu ya ukaguzi huru iliyofanywa na
wizara kuweza kuwabaini waliotelekeza mashamba, kambi ya upinzani inataka
serikali itoe msimamo juu ya taarifa ya ufuatiliaji wa mashamba na viwanda vya bidhaa na kilimo iliyofanyiwa kazi na
CHC kufuatia maelekezo waliyopewa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya
Umma (POAC).
Taarifa husika imebainisha kwamba mashamba 13
yenye ukubwa wa hekta 71,184 yalikuwa yameendelezwa kwa kiasi, wakati
mashamba 14 yenye ukubwa wa hekta 44,764 yalikuwa hayajaendeleza
kabisa/yametelekezwa! Mengi ya mashamba yakiwa ni mashamba ya Mkonge! Mashamba
hayo ni:-
1) Ndungu Sisal Estate, shamba hili lenye ukubwa wa
hekta 1,230. 9 liliuzwa kwa L.M investiment ya Tanga
mwaka 1997 kwa bei ya shilingi milioni 278 . Mpaka sasa 2012, miaka
15 baada ya kukabidhiwa shamba, mwekezaji
ameendeleza 52% tu ya shamba lote!
2) Mkumbara Sisal Estate , shamba hili lenye
ukubwa wa hekta 1,734
liliuzwa mwaka 1997 kwa M/S D.D Ruhinda & Company
LTD kwa bei ya shilingi 100
milioni. Mpaka sasa (miaka 15 baada ya kukabidhiwa shamba)
mwekezaji ameendeleza 52% tu ya shamba lote.
3) Toronto Sisal Estate, shamba lenye ukubwa wa
hekta 6,023 lililobinafsishwa kwa Highland
Estate Limited kwa bei ya shilingi milioni 265.4 mwaka 1998. Mpaka Septemba 2011, ni 50% tu ya shamba
lilikuwa limeendelezwa! Taarifa zilizopo ni kwamba mwekezaji husika hana hati
miliki ya shamba kutokana na kudaiwa riba
hivyo kushindwa kupata mkopo wa
kuliendeleza shamba.
4)
Magunga
Sisal Estate, shamba lipo wilaya ya Korogwe, lina ukubwa wa hekta 6,520. Katika shamba hili ambalo
linamilikiwa kwa ubia na kuendeshwa kwa kilimo cha mkataba kati ya wakulima wadogo
wa mkonge na Katani Limited limeendelezwa
kwa 19% tu .
5) Mgombezi Sisal Estate , shamba liko wilaya ya
Korogwe na lina ukubwa wa hekta 6,480 ambapo hekta 3881 zimegawiwa
kwa wakulima. Shamba linaendeshwa kwa kilimo cha mkataba kati ya wakulima wakubwa na wa kati. Eneo lililopandwa mkonge ni hekta 1301.6 tu!
6)
Hale
Mruazi Sisal Estate, shamba lina ukubwa wa hekta 4,180, ambapo hekta 1,136
tu ndizo
zilizopandwa Mkonge.
7)
Manzabay
Sisal Estate, shamba liliuzwa kwa Chavda
Group mwaka 1998. Mwekezaji alitumia hati miliki kupata mkopo
ambapo hakutumia mkopo husika kuendeleza shamba, shamba husika lilishikiliwa na
CRDB mpaka mwaka 2001 alipoiuzia Mbegu Technologies ambaye naye
amelikodisha kwa Omari Mduduma. Shamba halijaendelezwa!
8)
Kwashemshi
Sisal Estate, shamba lina ukubwa wa hetka
1498.5,shamba liliuzwa kwa Chavda
Group mwaka 1998, mwekezaji alitumia
hati miliki ya shamba kupata mkopo, ambao
hakuutumia kuendeleza shamba. Shamba
hilo lilishikiliwa na NBC mpaka 2003 lilipouzwa kwa Mathew Upanga Mnkande.
Shamba limeendelezwa kwa 35% tu!
9)
Ubena
Sisal Estate, shamba lenye ukubwa wa hekta
4,227 ambalo lipo wilaya ya Bagamoyo, mkoa wa Pwani liliuzwa kwa Highlands Estates Ltd mwaka 2007 kwa kiasi cha shilingi 278 milioni. Jumla ya hekta 499 ambayo ni
sawa na 12% tu imepandwa mkonge.
10)
Kingolwila
/Pangawe Sisal estate, shamba lenye ukubwa wa hekta 3703 liko wilaya ya Morogoro, mkoani morogoro, liliuzwa kwa Highland Estates limited kwa bei ya
shilingi milioni 210.2 kupitia PSRC
mwaka 2007. Jumla ya hekta 800 kati ya hekta 3703 ambazo ni sawa na 22% ya eneo
lote ndio limepandwa mkonge!
11)
Msowero
Sisal Estate, Shamba lenye ukubwa wa
hekta 5200 lipo wilaya ya Kilosa Morogogo , shamba liliuzwa na mamlaka ya Mkonge Tanzania kwa kampuni ya Noble Azania Agricultural
Enterprises mwaka 1993. Shamba
limepandwa mkonge hekta 900 tu ambazo ni
17% ya shamba lote na alizeti na
mtama zimepandwa hekta 200 tu. Hekta
4100 hazijaendelezwa toka mwaka 1993!
12)
Rudewa
Sisal estate, shamba lina ukubwa wa hekta 6351, liliuzwa kwa kampuni ya
Farm land mwaka 1992. Kampuni
husika iliuza shamba kwa kampuni ya
China State Farms Agribusiness (Group) corporation Tanzania Limited (CSFACOT) kwa kiasi cha dola za kimarekani milioni 1.2 mwaka 2000. Mwekezaji ameweza kuendeleza 32% tu kwa
kupanda mkonge hekta 2018 !
13)
Kimamba
Fibre Estate, shamba lenye ukubwa wa hekta 5743
liliuzwa kwa kampuni ya ANCO
ltd mwaka 1998. Mwaka 2009 Kampuni ya ANCO ltd iliuza hekta 3,043
kwa kampuni ya Sino na kubakiwa
na hekta 2700. Mustakabali wa shamba walilouziwa Sino
haujulikani, ila shamba lililobaki ANCO
ltd limeendelezwa kwa 46.3% tu!
Mheshimiwa
Spika, mashamba ambayo
hayajaendelezwa kabisa ni:
1)
Kikulu
Sisal estate ,lenye ukubwa wa hekta 5900 lililouzwa kwa Chavda Group, mwekezaji alieka dhamana shamba,kama kawaida yake
akachukua , mkopo hakuendeleza shamba.
2)
Kibaranga
Sisal Estate lenye ukubwa wa hekta 6,900, liliuzwa kwa kampuni ya katani ltd,
iliposhindwa kuendeleza serikali ililiweka chini ya PSRC na bodi ya
Mkonge.
3)
Kwamngwe
sisal estate, lenye ukubwa wa hekta 3700, liliuzwa kwa Chavda Group mwaka 1998,
alichukua mkopo, hakuendeleza shamba.
4)
Kwafungo
Sisal Estate, lenye ukubwa wa hekta 2310, liliuzwa kwa Chavda Group mwaka 1998, mwekezaji alitumia hatimiliki ya shamba kuchukua mkopo, ambapo hakutumia kwa
kusudi la kuendeleza shamba. Shamba hilo bado linashikiliwa na CRDB.
5)
Bombuera
Sisal Estate, lenye ukubwa wa hekta 2370, lipo Korogwe, liliuzwa kwa Chavda Group mwaka 1998. Mwekezaji
alitumia hatimiliki ya shamba kupata mkopo. Hakuliendeleza shamba. Mwaka 2002
CRDB iliuza shamba kwa AMC Arusha Ltd.
6)
Hale
Mwakiyumbi Sisal Estate, lenye ukubwa wa hekta 4,309. Shamba liliuzwa kwa Chavda Group, 1998. Alitumia hatimiliki kupata mkopo ambao hakuutumia kwa kusudi
lakuendeleza shamba na kulitekeleza. Shamba linashikiliwa na CRDB.
7)
Allidina Sisal estate, lenye ukubwa wa hekta 2300, liliuzwa kwa Noble Azania Agriculture Enterprises mwaka 1993. hakuna uwekezaji
wowote uliofanyika!
8)
Msowero (Godes) Farm, lenye ukubwa wa hekta
5,000. lilikuwa linasimamiwa na wizara
ya Kilimo chini ya Tanzania Livestock
research organization (TALIRO)
Mwaka 1993 serikali ya CCM ilipanga kujenga
chuo cha mifugo. Mpango ambao haukukamilika ,shamba likabaki bila
usimamizi wowote.
9)
Rutindi Sisal estate,lina ukubwa wa hekta 1,087. Shamba
liko Morogoro, linamilikiwa na
kampuni ya Noble Azania Agricultural
Enterprises. Shamba halijaendelezwa na mwekezaji toka amelinunua.
10)
Magole Sisal Estate, lina ukubwa wa hekta 1,149.
Lipo Dumira, kilometa 65 toka Kilosa.
Lilikuwa la serikali chini ya mamlaka ya mkonge
Tanzania. Japo halijabinafsishwa liko katika hali mbaya.
11)
Mauze Sisal Estate , lina ukubwa wa hekta 2,842.5. Shamba lilikuwa na deni la shilingi milioni 1.36 kutoka benki ya NBC.
Benki ilishikilia Hati miliki na
kuliweka chini ya ufilisi wa LART
kutokana na kuongezeka kwa deni mpaka milioni 10. Kwa sasa kuna
vijiji vya Kilangali na Mabwembele
vilivyoanzishwa na
vimesajiliwa ndani ya shamba. Halmashauri
za vijiji hivyo zinakodisha maeneo
katika shamba hilo kwa wanavijiji na watu kutoka nje ya vijiji kwa gharama ya shilingi
3,000 kwa ekari moja!
12)
Myombo na Kilosa
Sisal estate. Mashamba haya yenye ukubwa wa hekta 2,024 (Kilosa) na 1843
(Miyombo). Mashamba
yalibinafsishwa na mamlaka ya Mkonge
kwa Kampuni ya Katani mwaka 1998. Baada ya kampuni ya Katani
Limited kushindwa kuyaendesha ,iliyakodiha kwa kampuni
ya Agro-Focus. Mwaka 2005 Baraza
la Mawaziri liliagiza kuwa mashamba
haya yatafutiwe mwekezaji mwenye uwezo
kwani kampuni ya Agro- focus
LTD imeshindwa kuyaendeleza. Hata hivyo,
kinyume na maagizo mwaka 2009 Bodi ya Mkonge iliyauza mashamba haya kwa Agro-Focus.
Matokeo yake mpaka sasa hakuna uwekezaji wowote uliofanywa. Sehemu kubwa ya
shamba ni pori na sehemu iliyobaki imekodishwa
kwa wananchi kwa ajili ya kulima
mahindi.
13)
Madoto
sisal estate, shamba lina ukubwa wa hekta 3,200. Shamba lilinunuliwa na kampuni ya
SUMAGRO Ltd ambayo nayo ililiuza kwa East African Breweries mnamo mwaka
2009. Hakuna uwekezaji wowote
uliofanyika !
14)
Kivungu
Sisal Estate, shamba lina ukubwa wa
hekta 2,200. Shamba lilinunuliwa na
kampuni ya SUMAGRO Ltd. Mwaka 1998, ililiuza kwa East African
Brewaries mwaka 2009. Hakuna uwekezaji wowote uliofanyika!
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani
inaitaka serikali kuyarejesha mashamba yote ambayo wawekezaji wameshindwa
kuyaendeleza, kama ambavyo taarifa hii imevyoainisha. Hali kadhalika kwa wale
wawekezaji ambao wameweza kuendeleza sehemu ndogo na hawana uwezo wa
kuendeleleza shamba zima warejeshe sehemu ya mashamba waliyoshindwa kuendeleza ili
wapewe wananchi wenye uhitaji!
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani
inapendekeza serikali iangalie hatua za kuchukua dhidi ya wawekezaji katika
mashamba 13 ambao wafuatao wameshindwa kuendeleza mashamba kwa 100%. Pamoja na
wawekezaji katika mashamba 14 ambao wameshindwa kabisa kuendeleza mashamba
waliyonunua, kama ambavyo yameorodheshwa hapo juu.
Mheshimiwa Spika, kwa tathmini hii fupi
iliyofanywa na CHC utaona ni kwa namna gani zoezi la ubinafsishwaji mashamba
lilifanywa kiholela na kwa hujuma, pasipo kuzingatia maslahi ya umma. Katika
hali ya kawaida , watu wote walioshiriki katika zoezi hilo wana kila
sababu ya kuchukuliwa hatua, hakika
hawana tofauti na wahujumu uchumi. Kwa
mfano huyu ’mwekezaji’ anayejiita Chavda Group, aliuziwa shamba kwa bei ya kutupa mashamba saba, yenye ukubwa wa hekta 25,000, katika maeneo
tofauti ya nchi hii. Kikubwa alichokifanya ni kutumia hati za shamba kuchukulia
mikopo, kisha kutelekeza mashamba!! Hivi kweli unahitaji kuwa na akili nyingi
kuyaona haya? Nyuma ya Chavda Group wako akina nani?
Mheshimiwa Spika, ikumbukwe ni familia hii
hii ya Chavda ( V.G Chavda na kaka yake P.G Chavda),[5]
waliojitwalia mkopo wa $ 3.5m mwaka
1993 chini ya DCP (Debt Conversion
Program) wakiahidi kufufua mashamba ya
mkonge Tanga ndani ya miaka 10, na kupata $42 milioni. Walipopata hayo mapesa, hawakufanya lolote, na
hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi yao! Mheshimiwa Spika, kwa
utaratibu huu, lazima tuwachukulie wawekezaji wa aina hii kama ni ’waporaji’ na hawana tofauti na
majambazi yanayoiba benki kwa kutumia nguvu!
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka
serikali, kupitia Wizara ya Ardhi yenye jukumu pana la kusimamia sekta ya ardhi
kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo hayajaendelezwa na wawekezaji yanarejeshwa
serikalini bure bila fidia kwa ajili ya kutafuta wawekezaji wengine wenye mtaji
wa kutosha watakaoyaendeleza mashamba
hayo.
Hali kadhalika, kwa yale mashamba ambayo
tayari yana wakulima wadogo wadogo wanaoendesha shughuli zao za kilimo,
serikali ipange utaratibu wa kuwamilikisha wananchi maeneo husika, ili
kuondokana na ile dhana ya ’uvamizi’ au kukodishwa ardhi kwa ajili ya kilimo.
Zoezi hili lazima lifanywe kwa uwazi ili kuepuka udanganyifu uliotokea katika maeneo mengine ya nchi ambapo vigogo na watu wenye nafasi zao walijitwalia ardhi wakijifanya na wao ni
sehemu ya wanakijiji!
MASHAMBA YALIYOPENDEKEZWA
KURUDISHWA KWA WANANCHI MKOA WA ARUSHA
Mheshimiwa Spika, tarehe 17/6/1997 aliyekuwa Mkuu wa mkoa wa Arusha, Ndugu D. Ole
Njoolay aliitisha kikao
kilichohudhuriwa na Ndugu Kileo – katibu tawala Mkoa, Ndugu
P.H Muhale- Afisa Maendeleo ya ardhi (M), ndugu E. K. E Makere – Afisa
Ardhi na Ndugu Z.M.S Meirish – Afisa
Ardhi. Kikao husika kilichofanyika saa
4.35 asubuhi kilikuwa mahsusi kwa kuchambua mapendekezo yaliyoletwa kutoka wilayani kuhusu taarifa za mashamba makubwa mkoani Arusha.
Mheshimiwa Spika, mashamba yaliyojadiliwa na
kufikia maamuuzi mbali mbali yalihusisha wilaya sita:
a)
wilaya ya Arumeru- Mashamba 18
b)
wilaya
ya Ngoro Ngoro- Mashamba 10
c)
wilaya
ya Babati – Mashamba 11
d)
wilaya
ya Simanjiro – Mashamba 2
e)
wilaya ya karatu –Mashamba 6
f)
wilaya
ya Monduli – Mashamba 36
(Nakala ya Majina ya Mashamba pamoja na hatua
zilizopendekezwa nimeziambatanisha kama sehemu ya hotuba hii). Kambi ya
upinzani inaitaka serikali kulieleza Bunge hili tukufu nini mustakabali wa
mashamba 83, na hatua zilizochukuliwa kufuatia kikao husika.
Mheshimiwa
Spika, mwaka 1999, ofisi
ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, kupitia barua yenye kumb. Na. RC/AR/ CL 2/3 Vol
IV/19 ilimwandikia Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Arumeru
ikimtaarifu juu ya mashamba 11 ambayo yamepata kibali cha Rais kufuta miliki.
Taarifa ambayo ofisi ya mkuu wa mkoa ilipata toka kwa Katibu Mkuu
wa Wizara ya Ardhi kwa barua
yenye kumbu kumbu namba CL/46/VOL III ya tarehe
1 Juni 1999 .
Mashamba hayo:
1)
Shamba
namba 78 na 79 - NAIC , Usa River
2)
Shamba
namba 90 na 91- Madiira Coffee ltd
3)
Shamba
namba 98/2/1 – Duluti New – Duluti Lodge
4)
Shamba
namba 218/2- Maua limited
5)
Shamba la Oljoro – Salama estate
6)
Shamba
la Unit 15 Oljoro – Iman estate
7)
Karangai
Sugar Estate ( Tanzania Plantaion)
8)
Shamba
Namba 3 – Milimani pharmacy
9)
Shamba la Nduruma- Lucy estate
10)
Shamba
la Nduruma – Umoja Sisal Estate
11)
Shamba
la DOLLY – DOLLY ESTATE- FLYCATCHERS (ambalo
limegeuzwa uwanja wa Gofu na shamba la wanyama
kinyume na maagizo ya Rais)
Kambi ya upinzani, inaitaka serikali itupe
maelezo ya kina kuhusu mashamba haya!
MIGOGORO YA ARDHI
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tulifanya
katika mwaka wa fedha 2011/12, Kambi ya Upinzani itakuwa na utaratibu wa kila
mwaka wa fedha kuianishia serikali migogoro mbali mbali ya ardhi inayolikumba
taifa letu! Ni jukumu la Serikali kupitia vyombo vyake kuhakikisha kwamba
inafuatilia migogoro hii kwa kina na hatimaye kuyatafutia ufumbuzi:
BAGAMOYO- MKOA WA PWANI
Mheshimiwa Spika, wananchi wa kijiji cha Milo chenye
vitongoji vitano:- Milo, Relini, Kengeni, Kisiwani na Migude, kilichoandikishwa
chini ya sheria ya kijiji (chenye shule ya msingi na zahanati na kijiji)
wanailalamikia Kampuni ya Noble-Azania Agricultural Enterprises Limited ambayo
inadai ni wamiliki halali wa eneo hilo lenye ukubwa wa ekari 3000. Eneo ambalo
limekimeza kitongoji cha migude na sehemu ya kijiji cha milo. Kwa upande
mwingine, Kampuni ya Azania, inadai wanakijiji hao ni wavamizi kwa kuwa wao
wana umiliki halali wa eneo husika kupitia umiliki namba 36911.
WILAYA YA
MPANDA – KATAVI
Mheshimiwa Spika, mkoa mpya wa Katavi,
anakotoka Waziri Mkuu, ni kati ya maeneo yenye migogoro mingi sana ya ardhi,
mingi ikiwa ni migogoro sugu, ambayo imeshindwa kutafutiwa ufumbuzi licha ya
malalamiko kufika ngazi za juu serikalini pamoja na kamati ya ulinzi na usalama
ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Migogoro inazihusu kata za Kabwe na Korogwe, kijiji
cha Nkungwi[6],
kijiji cha Kabange, Kijiji cha Mbuguni, mgogoro baina ya hifadhi ya Ubende na vijiji
kumi na nane.
Mheshimiwa Spika, nitawasilisha mezani kwako
nyaraka mbali mbali za migogoro hii, kama serikali itaona inafaaa, iyafanyie
kazi!
Mheshimiwa Spika, kutokana na muda, nitaelezea
mgogoro mmoja sugu, ambao unahusisha watendaji serikalini. Mgogoro ambao unaambatana na vitisho kwa wananchi, mpaka
kufikia hatua wananchi kufunguliwa kesi za jinai[7] ili
kuwatisha. Wananchi wa Kata ya Sibwesa,
wilaya ya Mpanda wanalalamikia mtandao ambao umeundwa na watumishi wa serikali,
ambao ni waajiriwa wa Halmashauri ya
Wilaya ya Mpanda, wanaofahamika kama Cletus Siwezi, Andrea Malando (Kitengo cha
Ardhi) na Bwana Galus Kasonso (Meneja wa mradi wa maji katika Halmashauri ya Mpanda ).
Mheshimiwa Spika, watumishi hawa
wanalalamikiwa na wananchi, wakituhumiwa kuwanyang’anya mashamba yao kwa kutumia nafasi zao.
Mheshimiwa Spika, mtumishi huyu wa Serikali
(kupitia kwa bwana Ramadhani), alishindwa kuthibitisha umiliki wake katika
baraza la ardhi la Kata, walikimbilia Baraza la Ardhi na Nyumba la Sumbawanga
ambapo ilitolewa hukumu ya upande mmoja! Baada ya hukumu hiyo ya upande mmoja
kumekuwa na hujuma dhidi ya wananchi na kuna malalamiko kwamba kuna mbinu ya
kuandikwa hati ya kukamata heka mia tatu na sitini (360) kutoka mbuga ya Mwamapuli, kijiji cha Kabage na mbinu yake ya kuendelea
kufanya mipango ya kukamata watu bila ya kuwa na kosa kwa kutambua kuwa hawana
uwezo wa kukabiliana na kesi za jinai.
Jeshi la polisi linahusishwa pia katika mazingira mawili, la kwanza kufungua
kesi za kubambikiza, hali kadhalika kumlinda mhalifu!
Mheshimiwa Spika, yanayotokea Mpanda,
yanafanyika pia kwenye maeneo mengi ya nchi hii, kwa watu ambao wamepewa
dhamana kutoa huduma hii muhimu kwa wananchi, kutumia fursa hiyo kujilimbikizia
ardhi, na pale ambapo wananchi wa kawaida wenye uhitaji wa huduma hiyo kukumbana na urasimu
mkubwa uliotawaliwa na rushwa!
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inaitaka
serikali ijipime kwa kuangalia ni hatua gani stahili itawachukuliwa watumishi
hao wa halmashauri kama ushahidi ulivyotolewa, na pengine inaweza pia kubaini
mambo mengi mazito yaliyojificha!
MKOA WA MANYARA- BABATI
Mheshimiwa Spika, mgogoro huu unahusu hifadhi ya Taifa Tarangire na Vijiji
vya Gijedabung, Ayamango[8] na
Gedamar[9].
Mheshimiwa Spika, vijiji hivi vilikaliwa
na wananchi toka miaka ya 1960. Hifadhi ya Tarangire ilianzishwa mwaka 1970 kwa kuzingatia tangazo la
Serikali (GN) Na. 160. Mipaka yake ilitambulishwa kwa barabara
iliyozunguka hifadhi nzima na
kuipatia umbo linaloonekana katikati
yake kupitia Sheria ya mwaka 1974 ya
Vijiji na Vijiji vya ujamaa, mpaka ambao wananchi wote waliutambua na
kuuheshimu.
Mheshimiwa
Spika, mgogoro ulianza baada ya uongozi wa hifadhi
ya Tarangire ulipotekeleza zoezi
lake la kuhakiki mipaka yake kwa nia ya kufanya tafsiri yakinifu kwa kutumia
vifaa vya kisasa. Wataalam walibaini kwamba ule mpaka wa miaka yote wa barabara,
ulioliwekwa na Mamlaka ya Hifadhi
yenyewe haukuzingatia vipimo halisi na hivyo kusababisha eneo lenye ukubwa wa ekari 16,249.10325 kuingizwa kwenye mamlaka
ya vijiji kimakosa. Kwa mantiki hiyo hifadhi iliamuru wananchi waliokuwa wakiishi kwenye ardhi hiyo kuhama mara moja na kusitisha matumizi yote juu
ya ardhi hiyo.
Mheshimiwa
Spika, kutokana na amri
hiyo, wananchi wengi wa maeneo haya wako katika hali mbaya sana kiuchumi
kutokana na ardhi waliyokuwa wanaitegemea kuchukuliwa na serikali! Wananchi
wamezuiwa kufanya kitendo chochote cha kufanyia matengenezo makazi yao
walioishi kwa zaidi ya miaka 50. Ikumbukwe kwamba wananchi hawa hawakuvamia
eneo hili bali waliwekwa na mamlaka ya wilaya kwa makosa pasipo kukusudia. Pamoja na serikali kutaka
kuwahamisha wananchi hao haijafanikiwa kuwapatia makazi mapya na mashamba ya kulima.
Mheshimiwa
Spika,usumbufu wa
Askari wa Hifadhi ya Tarangire wanaofanya vitendo vya
unyanyasaji ni kero kubwa kwa usalama, utulivu
na ustawi wa wananchi wa maeneo
husika. Kambi ya upinzani haidhani kwamba hifadhi ni muhimu zaidi kuliko watanzania waliokiweka
CCM madarakani. Ni rai yangu kwa Rais wa
Jamhuri ya Muungano awatazame wananchi wa maeneo haya kwa jicho la huruma! Awatazame wananchi wa maeneo haya kwa jicho
la huruma kutokana na kwamba hawana maeneo mbadala ya kuishi ili kuendeleza
maisha yao! Rais wa Jamhuri ya Muungano
ana mamlaka ya kuhawilisha ardhi ya Hifadhi
ya Taifa ya Tarangire inayokaliwa na
wananchi wa vijiji tajwa ili iwe
ardhi ya kijiji, ombi ambalo lilisha
wasilishwa Wizara ya Ardhi Nyumba na Makazi, lakini mpaka leo hakuna majibu!
MKOA WA KAGERA- wilaya ya Karagwe
Mheshimiwa
Spika, muda sasa Kambi ya Upinzani, pamoja na wabunge
wengi, wamekuwa wakizungumzia juu ya mgogoro baina ya wakulima na wafugaji,
kutokana na serikali kutokuwa na mpango endelevu wa kutenga maeneo ya wakulima
na wafugaji. Mwaka jana katika hotuba ya Kambi,
tulielezea juu ya mgogoro wa wakulima na wafugaji wa jamii ya Wamasai katika eneo
la vijiji vya Izava (Chamwino) na Chitego (Kongwa). Mgogoro huu mpaka
leo hujapatiwa ufumbuzi. Kimsingi mgogoro
ulisababishwa na ubabe na maamuzi mabovu ya mkuu wa wilaya. Katika hotuba hii, Kambi
ya Upinzani inafikisha mbele ya Bunge lako Tukufu kilio cha wanavitongoji vya Karugwebe, kijiji cha ITEERA na kitongoji cha MTAKUJA kijiji cha
CHANYA, Karagwe.
Mheshimiwa
Spika, wananchi
wanalalamikia kufukuzwa kwenye maeneo yao ya kilimo na kupewa wafugaji
matajiri bila wao kuhusishwa! Baada ya
kufukuzwa hawakupewa hifadhi, kitu ambacho kimewafanya wawe wahamiaji wasio
rasmi ndani ya nchi yao! Ikumbukwe wananchi hawa walikuwa wanafanya shughuli za
kilimo kwa kipindi cha zaidi ya miaka 20. Madiwani walipohoji katika kikao cha
baraza la madiwani kilichofanyika ntarehe 31/2/12, walipata vitisho kutoka kwa
Mkuu wa wilaya ya Misenyi aliyekuwa
anakaimu ukuu wa wilaya ya Karagwe!
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani
inataka kauli ya serikali kuhusiana na matukio haya mawili; hali kadhalika
serikali ilitaarifu Bunge lako tukufu, ni lini Serikali itaandaa mpango rasmi
wa matumizi ya ardhi kwa wakulima na wafugaji ili kuepuka migogoro isiyokwisha!
MKOA WA DAR- ES- SALAAM
Maeneo ya Pembezoni
Mheshimiwa
Spika, miaka ya hivi
karibuni serikali imekuwa na mikakati, inayoitafsiri kama mikakati kabambe ya kuendeleza
maeneo yaliyomo pembezoni mwa jiji la Dar es salaam. Mipango hiyo imeleta msiba
mkubwa sana kwa wananchi wa maeneo hayo! Kwa sababu ya muda, tutazungumzia
miradi ya Luguruni na Kwembe Kati, Kinondoni Dar es salaam.
Mheshimiwa
Spika, katika maeneo
haya, wananchi wameporwa ardhi yao yote
kwa fidia ndogo sana, wamebomolewa makazi yao na kutimuliwa kutoka kwenye ardhi yao kwa nguvu ya dola, wakiwa wamemaskinishwa
kupindukia baada ya kuporwa rasilimali ardhi yao, na wakiwa na fidia
duni mkononi, wakihamia kwingineko kuanzisha
makazi yasiyopimwa na ya kimasikini kupindukia!
Miradi hiyo imegubikwa na utendaji wenye kupindisha sheria, ubabe, usio
na utawala bora, ulioteteresha viwango
vya ramani na upimaji uliochakachua
fidia, uliofanya ofa na hatimiliki kuwa
uyoga, uliojaa dhuluma na hujuma dhidi
ya hakiardhi ya wananchi.
Hapo Luguruni tarehe 22/5/2007 Mkurugenzi wa Makazi
na Ardhi alitangaza utwaaji wa
ardhi wa 5% ya Ardhi kwa ajili ya
miundombinu. Hali hii ilibadilika
kufikia 100% na waliofanya hivyo ni watendaji wa mradi baada ya mkurugenzi
husika kustaafu.
Mheshimiwa
Spika, hali kadhalika
kinachofanyika Kwembe Kati,
kwa maeneo ya miundombinu, biashara na makazi yalitwaliwa
na Mradi na kutangazwa kuwa mali ya serikali, licha ya tamko la Waziri wa Ardhi Mhe. Chiligati Bungeni la
tarehe 18/06/2009 na tamko la Naibu Waziri wa Ardhi Mhe. Goodluck
Olemedeye Bungeni tarehe 12/11/2011 kusisitiza ya kwamba baada ya Rais
kutwaa ardhi na Miundombinu albaki ya ardhi kwa ajili ya makazi na biashara ibakie
mikononi mwa wananchi wamiliki wa
ardhi, waiendeleze wao wenyewe ili
waweze kujikomboa kiuchumi.
Katika maeneo yote hayo, baada ya ardhi yote ya
wananchi kutwaliwa kwa fidia duni chini ya 20% ya bei ya soko kinyume hata na
matakwa ya sheria ya ardhi, namba 4 ya mwaka 1999, sehemu ya II, kifungu cha 3
kinachoelezea misingi mikuu ya sera ya ardhi ya Taifa, wananchi walitimuliwa
kimabavu baada ya makazi yao kubomolewa kwa tingatinga. Mfano dhahiri ni
wa eneo la Luguruni; fidia iliyolipwa kwa
mita moja ya mraba ilikuwa ni shilingi
1,977, ardhi hiyo hiyo iliuzwa kwa tshs
30,000 mita moja ya mraba bila
maendelezo yoyote! Hivyo kuzalisha faida ya 1500% …Huu ni wizi na unyonyaji
mkubwa.
Mheshimiwa
Spika, inasikitisha sana
pale watendaji wa wizara ya Ardhi,
wanapotumia mgongo wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kutengua toleo la hatimiliki halali za wananchi wamiliki wa ardhi, kupora ardhi yao kwa mtindo huu, kupima viwanja
vipya juu ya viwanja vya awali.
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani inataka
serikali hii ya CCM, kuacha kufanya mambo kibabe, na kusitisha kile
kinachoendelea katika maeneo ya Luguruni na Kwembe Kati. Ulipaji fidia unakuwa na mianya lukuki
ya ubadhirifu wa fedha, hivyo kuhitaji ukaguzi na udhibiti wa makini sana wa masuala
yote ya malipo na matumizi ya fedha kwenye miradi ya Luguruni na Kwembe Kati. Viwango vya fedha vinavyohusika hapa ni vikubwa sana kutokana na wingi wa watu wanaohitaji kufidiwa na kutokana na mauzo ya viwanja
vilivyopatikana katika mchakato mzima wa
kutwaa na kuuza ardhi, kuna uhitaji mkubwa wa ukaguzi na udhibiti mahsusi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu.
Suala la ukaguzi ni muhimu kutokana na tuhuma kwamba malipo ya fidia yamefanywa
bila kutumia nyaraka halali
za matayarisho na ulipaji fedha .
Tatizo la Uvamizi wa Maeneo ya watu
Mheshimiwa Spika, kuna tabia iliyozuka kwa
kasi sana, katika manispaa ya Kinondoni, hususan maeneo ya pembezoni, na katika
jimbo la Kawe; ninaloliwakilisha tabia hii imekithiri sana kata za Bunju,
Mabwepande na Wazo. Kumekuwa na genge la watu wenye silaha wanaovamia maeneo ya watu, kuharibu mali,
kugawa viwanja na kuwauzia watu (wapya) viwanja kwa bei ya kutupa . Hilo genge,
baada kufanya uharibifu eneo moja, huhamia eneo lingine! Hali hii imesababisha uvunjifu wa amani, na katika
mazingira mengine kusababisha vifo!
Mheshimiwa Spika, hofu ya wananchi inaongezeka
kutokana na kutokupata ushirikiano kutoka kwa mamlaka zenye jukumu la kuhakikisha
wananchi na mali zao wako katika hali ya usalama. Kamati ya ulinzi na usalama
ya wilaya na Mkoa wa Dar es salaam zote
zina taarifa ya genge hili la majambazi
wa ardhi, vyombo mbalimbali vya habari vimetoa taarifa kuhusu genge hili la
majambazi, hakuna hatua zilizochukuliwa
na wala hakuna dalili kama kuna dhamira ya dhati ya kuweza kutafuta suluhu!
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kwamba serikali
ingejipanga katika matumizi bora ya ardhi na kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata ardhi kwa gharama nafuu
bila urasimu walarushwa, hili genge la
majambazi wa ardhi lisingepata wateja!
Kambi ya Upinzani inaitaka serikali ieleze
Bunge ina mipango gani ya muda mfupi na mrefu kuweza kukomesha kabisa suala la
uvamizi wa maeneo ya wazi! Nikiwa mbunge wa Kawe, napenda kuwasisitizia
wamiliki wote wa ardhi Jimbo la Kawe, serikali ya wilaya kupitia kamati yake ya
ulinzi na usalama imeshindwa kuwapa ulinzi wenu na mali zetu. Niendelee
kuwashawishi kila mmoja kwa nafasi yake mmoja mmoja au kwa vikundi kuweka
walinzi binafsi kwa ajili ya kulinda mali zao! Na chochote kikitokea mbunge
wenu nitawalinda kwa sababu nilishatoa taarifa kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa
mpaka serikali kuu!
Majiji ya Viungani (setelite towns)
Mheshimiwa Spika,
Mwaka 2006/07 Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
ikishirikiana na Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam na Manispaa zake tatu
ilianzisha Mkakati wa kuanzisha miji midogo sita itakayokuwa na vituo vya
huduma za kijamii na za kibiashara. Kutokana na ukubwa wa mpango huo iliamuliwa
kuwa utekelezaji uanze katika eneo la Kibamba Luguruni ambalo lilipaswa kuwa
eneo la mfano ambapo uzoefu katika uendelezaji ungetumika kwa maeneo mengine ya
Jiji na nchi nzima kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika, Uanzishwaji
wa Mji wa Kibamba uligawanywa katika maeneo makubwa matatu: Eneo Kitovu cha Mji
cha Luguruni, eneo la makazi mbadala la Kwembe Kati na uendelezaji wa eneo
linalozunguka kituo. Hata hivyo miaka zaidi ya mitano imepita bila uendelezaji
huo kukamilika na hivyo sehemu kubwa ya maeneo tajwa kurejea kuwa mapori na
kuanza kurejea kwa migogoro ya ardhi katika maeneo tajwa.
Mheshimiwa Spika,
Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kueleza matokeo ya tathmini ya
utekelezaji wa mpango huo na kueleza bayana kasoro na matatizo yaliyojitokeza
sambamba na kuharakisha ujenzi wa mji husika ili kuwa mfano kwa mipango ya
ujenzi wa miji mingine ambayo maandalizi yake yanaelezwa kutaka kufanyika
katika mwaka wa fedha 2012/2013.
Mheshimiwa Spika, wakati zoezi la wa Luguruni, Kwembe Kati na Kigamboni
yakitawaliwa na malalamiko makubwa sana kutoka kwa wananchi, Wizara ya Ardhi na
Maendeleo ya Makazi imeandaa mpango mpya
wa Makongo. Mradi huu utasimamiwa
na mtendaji aliyeendesha zoezi la kihuni la ujenzi mpya wa mji wa Kigamboni!
Kambi ya Upinzani inaona mradi huo umeanza
vibaya kwani msimamizi wake mkuu haaminiki kutokana na miradi aliyoisimamia
huko nyuma. Hivyo basi inaitaka Serikali ikutane na wananchi
na majirani zake wa Makongo tulijadili hili kwa kina! Kutumia mabavu
hakutasaidia! Wananchi wa makongo wanataka maendeleo, lakini yasiwe maendeleo
yenye lengo la kuwapa mzigo, ufukara na kuwahamisha wale ambao hawatakuwa na
uwezo wa kukidhi matakwa ya mradi! Nasisitiza mimi ni mbunge wako, njoo
tuzungumze!
UWINDAJI, UFISADI NA UKIUKWAJI WA SHERIA ZA MATUMIZI YA ARDHI
Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sasa Ardhi ya
Tanzania imegeuzwa shamba la bibi na kikundi cha mafisadi! Kambi
ya Upinzani
imeshuhudia mkataba ulioingiwa baina ya
kampuni za Uranium resourses
PLC, Western Metals Limited na
Game Frontiers of Tanzania Limited.
Mkataba ambao umetengenezwa na Kampuni ya Kitanzania ya REX ATTORNEYS. Na
ulisainiwa tarehe 23.3.2007.
Mheshimiwa
Spika, mkataba husika,ambao
vipengele vyake vinaainisha kwamba unatakiwa uwe wa SIRI unaihusu kampuni ya
uwindaji, inayofahamika kwa jina la Game Frontiers of Tanzania Limited inayomilikiwa na Bwana Mohsin M. Abdallah na
ndugu Nargis M. Abdallah. Kampuni
hii ya uwindaji, imeingia mkataba na kampuni mbili za kigeni, za kufanya
utafiti wa uchimbaji wa madini ya Uranium katika kijiji cha Mbarang’andu kwa
malipo yafuatayo:-
a)
Malipo
ya $ 6,000,000/- za kimarekani, ambazo zitalipwa kwa awamu mbili ya malipo ya
$3,000,000. Malipo ya kwanza yatafanyika pale uzalishaji wa urani utakapoanza.
b)
Malipo
ya $ 250,000/- baada ya kampuni za madini kukamilisha utafiti wa madini ya urani
na kupata kibali cha uchimbaji wa madini.
c)
Malipo
ya $ 55,000 kila mwaka kama fidia ya kushindwa kufanya biashara na usumbufu
unaotokana na shughuli za machimbo kwenye kitalu! Malipo hayo yatafanyika kila
tarehe 31 Machi.
d)
Malipo ya $ 10,000 kwa vijiji vitakavyoathiriwa
na utafiti huo wa urani. Malipo ambayo yametokana na makubaliano baina ya
kampuni ya uwindaji na kampuni za madini!
Mheshimiwa
spika, nimepitia sheria
za uhifadhi wa wanyamapori, The wildlife Conservation Act, 1974 (Sheria ya zamani)
na Sheria mpya The wildlife Conservation Act, Act no 5 of 2009. Sheria hizi
zinamruhusu mtu aliye na leseni ya uwindaji, kuwinda wanyama tu!
Mheshimiwa
spika, hali kadhalika,
Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1999, Sheria namba 4 ya mwaka 1999 na Sheria ya Ardhi
ya vijiji, sheria namba 5 ya mwaka 1999 inatamka bayana kwamba ardhi inajumuisha
vitu vyote vilivyo juu ya ardhi na chini ya ardhi isipokuwa madini au mafuta………
Na kwa mujibu wa sheria za Tanzania linapokuja suala la madini, umiliki unatoka
kwa mtu binafsi na kurudi serikalini! Na ni Serikali kupitia Wizara ya Nishati
na Madini ndiyo pekee yenye mamlaka ya kutoa leseni ya kutafuta madini kwa
kampuni za madini!
Mheshimiwa
Spika, Kambi ya Upinzani
inaitaka serikali ilieleze Bunge lako tukufu uhalali wa mkataba kati ya Game
Frontiers na Uranium Resourses PLC na Western Metals! Ni sheria ipi inayoipa
kampuni ya uwindaji haki ya kualika kampuni ya nje kwenye eneo ambalo haina
umiliki kufanya utafiti na hatimaye kuchimba madini hatari kama urani? Nini
mustakabali wa Watanzania wanaoishi kwenye vijiji vinavyozunguka mbuga hiyo
ambao wanaishi maisha yao ya kila siku pasipo kujua kama kuna utafiti wa madini
hatari ya urani unaoendeshwa kwa siri kubwa? Ni serikali ya aina gani, yenye
uwakilishi mpaka ngazi ya kitongoji na usalama wa taifa mpaka ngazi za chini
kabisa za utawala inashindwa kuyaona haya?
MCHAKATO WA KUTOA ARDHI KWA
WAWEKEZAJI
Mheshimiwa Spika, uchunguzi uliofanywa na haki ardhi
umebaini kuwa katika wilaya ya Kilwa, mwekezaji alikuwa na kampuni iitwayo
Bioshape kutoka nchini Uholanzi. Kampuni hii ilipewa ardhi yenye ukubwa wa
hekta 80,000 kwa lengo la kulima zao la mbono kaburi, ardhi hiyo ilihusisha
vijiji vinne ambavyo ni Mivuji, Migelegele, Liwili na Inokwe. Mwekezaji
hakutumia eneo lote na kulima hekta 800 tu katika kijiji cha Mavija ambazo
ziligeuka kuwa pori baada ya mwekezaji kutelekeza shamba, vifaa na wafanyakazi.
Mheshimiwa Spika, katika wilaya ya Kisarawe,
mwekezaji alikuwa ni kampuni inayoitwa SunBiofuels kutoka nchini Uingereza.
Kampuni ilipewa ardhi ya ukubwa wa ekari zipatazo 9000 iliyojumuisha ardhi za
vijiji 11 ambavyo ni Marumbo, Muhaga, Mtamba, Mzenga A, Kurui, Chakenge,
Mitengwe, Paraka, Kidugalo, Vilabwa na Chakaye. Mwekezaji huyu hakulima shamba
lote bali alilima shamba la mfano katika eneo la ekari zipatazo 3000 lililopo
kijiji cha Mtamba ambalo lilikuwa na mazao ambayo mengi yameanza kuzaa matunda
huku yakiwa tayari kwa kuvunwa, pia Bagamoyo kampuni iliyohusika inaitwa Sekab
Bioenergy Tanzania Limited.
Mheshimiwa Spika, ieleweke kuwa katika maeneo yote
ardhi zilikuwa za aina mbili; zilizomilikiwa na wanakijiji na zile za vijiji
ambazo zilipaswa kuhawilishwa kwanza na kisha kutolewa kwa mwekezaji. Kwa
jumla, wananchi katika vijiji, watendaji wa vijiji, wajumbe wa kamati za vijiji
kwa pamoja walisema hawakuridhika na mchakato uliotumika kutoa ardhi kwa
wawekezaji.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani inasikitika mchakato kujaa mizengwe, hadaa, utapeli kwa wananchi na hata
harufu ya rushwa kwa baadhi ya watendaji wa vijiji, maofisa ardhi katika wilaya
na vigogo wa juu katika wilaya na halmashauri. Hata pale ambapo wananchi
walirubuniwa kutoa ardhi zao kwa kuelezwa kuwa mwekezaji ataleta neema katika
maeneo yao, bado fidia hazikuwafikia, zilichelewa au fidia iliyotolewa ilikuwa
ndogo, huku zoezi la kutathmini mali zilizopo katika ardhi zao likiwa siyo la
wazi na shirikishi. Hata vigezo vya tathmini kwa ardhi na mazao havikuwekwa
bayana kwa pande husika.
Mheshimiwa Spika, Kambi ya Upinzani kwa niaba ya
wananchi inaitaka serikali kuzingatia sheria na kusimamia utekelezaji wake kwa
ngazi mbalimbali kwa kuwatendea haki wananchi kuwapa huduma zenye uhalali
kisheria ikizingatiwa fidia zilizotolewa hazikurandana na hali halisi ya soko
kwa wakati husika.
Mheshimiwa
Spika,Serikali katika
hotuba yake hapa bungeni kupitia Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi mwaka
wa fedha 2011/12 ilikiri kuwa na
changamoto ya kutokuwa na mfumo thabiti
na utunzaji wa kumbukumbu za sekta ya ardhi na kutoa ahadi ya kujenga mfumo
mmoja wa kuhifadhi kumbukumbu za ardhi kwa njia ya kielekroniki (Integrated
Land Management System) utakaounganisha mifumo yote ya utunzaji wa
kumbukumbu za sekta ya ardhi. Kambi ya Upinzani inaitaka serikali kueleza wananchi
mfumo huu umefikia wapi na utekelezaji wake uko je?
Mheshimiwa
Spika, kutokana na
tatizo la ardhi kwa maana ya uwekezaji na matumizi mbalimbali ya serikali
kutopatikana kwa urahisi mijini na
vijijini, serikali kupitia wizara iliahidi hapa bungeni kuanzisha chombo
kitakachosimamia hazina ardhi (Land Bank) ili kurahisisha upatikanaji wa ardhi
kwa ajili ya miradi ya uwekezaji na kuunda mfuko wa kulipa fidia(Land
Compensation Fund) kwa mujibu wa sheria za ardhi ili kuiwezesha serikali kulipa
fidia timilifu na kwa wakati inapotwaa ardhi kwa maslahi ya umma. Kambi ya
Upinzani inataka kupata majibu kutoka kwa serikali ni hatua gani ziliendelea kuchukuliwa
ikizingatiwa kuwa tatizo la fidia limeendelea kuwepo na kuwa kero kwa wananchi?
SEKTA YA NYUMBA
Mheshimiwa Spika, sekta hii ni sekta pekee inayoweza kuleta na
kutekelezwa kwa dhana nzima ya maisha bora kwa kila Mtanzania. Nchi yetu na Watanzania
kwa ujumla bado tuna matatizo makubwa ya nyumba bora na za bei nafuu kutokana
na bei kubwa ya simenti na bati- bidhaa muhimu katika kutimiza azma ya ujenzi.
Mheshimiwa Spika, tulisema na tunasema kuwa bei ya simenti na bati
inaweza kuwa chini ya shilingi elfu saba, kama serikali itakuwa na utashi wa
kuwahudumia wananchi kwa dhati. Bei ya
simenti Uturuki na Paksitani
ukinunua tani 600,000 bei ya tani moja ni dola za Marekani 70 hadi bandarini.
Guangzhou –China tani moja ni dola za marekani 26. Kwa hesabu za kawaida kwa
mfuko mmoja ni dola 3.5 sawa na shilingi
5250/- kama ukinunua Pakstani au Uturuki. Ukinunua China bei itakuwa dola 1.3.
sawa na shilingi 1950/-
Mheshimiwa Spika, Kambi ya
Upinzani bado inasisitiza kuwa kama Serikali ina dhamira ya kweli mfuko wa
simenti hauwezi kuuzwa zaidi ya shilingi 7,500. Hivyo basi tunaitaka Serikali
itueleze kwa nini bei ya simenti inauzwa zaidi ya shilingi 14000 Dar es salaam
na nje ya Dar es Salaam bei ni zaidi ya hapo, wakati malighafi zinapatikana
hapa hapa nchini na kiwanda kikubwa cha simenti kinatumia gesi asili ili
kupunguza gharama za umeme.
Mheshimiwa Spika, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza gharama
hizi na ni faida kiasi katika kodi tunayopata kwa kuwalangua Watanzania.
Serikali haioni kwamba ina wajibu wa
kuondoa hizi kero wananchi wajenge nyumba bora na kwa bei nafuu?
SHIRIKA LA NYUMBA LA TAIFA
Mheshimiwa Spika, Shirika la Nyumba la Taifa, lilipoanzishwa mwaka 1962, moja kati malengo yake ilikuwa ni kujenga nyumba za bei nafuu kwa
ajili ya Watanzania wafanyao kazi mijini . Hata hivyo kwa kadiri siku zilivyosonga mbele, shirika hili liligeuka kutoka
kuwahudumia masikini na watu wenye kipato cha kati na badala yake linawahudumia
watu wa kipato cha juu.
Mheshimiwa Spika, Shirika la Nyumba la Taifa linahudumia asilimia
0.5 tu ya watanzania wote wa nchi hii. Swali
la msingi ni je Serikali imeweka mikakati gani ya kuhakikisha kuwa shirika hili
linahudumia Watanzania wengi zaidi kwa kuwapatia nyumba za bei nafuu?
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2011/2012 Kambi Rasmi ya Upinzani imepata taarifa kuhusu
ujenzi inaoendelewa kufanywa na Shirika la Nyumba katika maeneo mbalimbali
nchini. Kambi rasmi ya upinzani inataka Wizara kutoa maelezo kwa umma kuhusu
migogoro iliyojitokeza kati ya shirika na wapangaji na hatua ambazo
zimechukuliwa kushughulikia malalamiko yaliyotolewa hususan katika maeneo ya
Chang’ombe, Ubungo na mengineyo.”
KODI YA ONGEZEKO LA THAMANI (VAT) NA ONGEZEKO LA MTAJI (CAPITAL GAIN TAX) KWENYE
MAUZO YA NYUMBA ZINAZOJENGWA NA SHIRIKA
Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa inayowakabili Watanzania wengi
ni kuweza kupata nyumba za bei nafuu. Suala hili tulilizungumza mwaka jana, na
tutaendelea kulizungumza! Kwa sheria zetu za kodi, nyumba mpya iliyojengwa kwa
ajili ya kuuzwa inapaswa kutozwa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) pale
inapouzwa, na anayelipa kodi hiyo ni mnunuzi!.
Mheshimiwa Spika, suala la
msingi ni kuwa nyumba hiyo wakati inajengwa vifaa vyote vya ujenzi vililipiwa
kodi hiyo, hivyo kitendo cha mnunuzi kulipa kodi ya VAT wakati wa kununua
nyumba hiyo ni kulipia kodi mara mbili (DOUBLE TAXATION). Je, serikali haioni
kama haimsaidii mwananchi kuweza kuishi kwenye nyumba nzuri na kwa gharama
iliyo nafuu?
Mfano dhahiri ni kwamba kwa
mwaka wa fedha 2010/11 shirika lilitarajia kujenga nyumba 49, zenye jumla ya thamani ya shilingi
bilioni 4.08. Kwa gharama iliyotumika, wastani wa nyumba moja ililigharimu shirika shilingi milioni
83.4.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya
utekelezaji wa Kazi za Shirika la Nyumba la Taifa kuanzia Julai 2010 hadi Mei 2011 walitarajia
kupata shilingi bilioni 6.3 kutokana
na mauzo ya nyumba hizo, yaani faida ya
shilingi bilioni 1.9 Kwa tafsiri nyingine nyumba moja itauzwa
na shirika la nyumba kwa shilingi milioni 129.2, wakati gharama halisi
za ujenzi ni shilingi milioni 83.
Kwa kila nyumba iliyouzwa shirika limepata faida ya shilingi
milioni 46.
Mheshimiwa Spika, sheria ya mikopo yaani "Government
Loans, Guarantees and Grants Act 1974 and amendments 2003" inalifanya
shirika la nyumba la taifa kulazimika kupata kibali kutoka Wizara ya Fedha hata
pale ambapo halihitaji kupata dhamana ya serikali na pia hata kwa mikopo ya
ndani ya nchi. Wote tunafahamu rasilimali ambazo shirika hili linazo. Pamoja na
kufahamu yote, bado tumeamua kuliweka shirika hili katika urasimu mkubwa wa
kiserikali wa kupata vibali kutoka wizara ya fedha bila ya sababu za lazima.
Je, serikali imedhamiria kutekeleza ahadi zake katika ujenzi wa nyumba na
kuliwezesha shirika kujiendesha kibiashara kama sheria yake inavyolitaka? Kambi
ya Upinzani inaitaka serikali itoe ufafanuzi ni lini inatarajia kuanzisha
mchakato wa kurekebisha sheria hiyo?
MAMLAKA YA/WAKALA WA
KURATIBU BEI ZA PANGO LA NYUMBA
Mheshimiwa Spika, katika
hotuba ya Kambi ya Upinzani kwa mwaka wa fedha 2011/2012 tuliitaka serikali
kuanzisha chombo kitakachoweka utaratibu utakaotambulika kisheria ili kiwe kinatoa miongozo
ya kudhibiti gharama za kodi za nyumba
kwa ujumla wake. Kwa
maana nyingine ni kuanzisha mamlaka ya udhibiti itakayoitwa”Real Estate
Regulatory Authority”. Tunarudia
tena kusisitiza ushauri wetu huo.
Mheshimiwa Spika, sekta hii ambayo imejaa
changamoto ambazo kama zikifanyiwa kazi ni dhahiri pato la taifa litaongezeka
na pia tatizo la ajira linaloikabili nchi yetu linaweza kupungua kwa kiasi
kikubwa kama si kuondoka kabisa. Swali muhimu la kuuliza ni kwa vipi Serikali
itabadilidha changamoto kuwa fursa?
Kambi ya Upinzani inaitaka Serikali
kuangalia kwa makini kuwa mamlaka ya udhibiti ndiyo inayoweza kubadilisha
changamoto zilizopo katika sekta hiyo kuwa fursa.
Mheshimiwa Spika, ninawashukuru
waheshimiwa wabunge wote kwa kunisikiliza na naomba kuwasilisha.
................................................
Halima James Mdee(Mb)
Msemaji Mkuu wa Kambi ya
Upinzani- Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi.
11.07.2012
No comments:
Post a Comment